1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaHaiti

Mji wa Port-au-Prince wakumbwa na mashambulizi mapya

Zainab Aziz
21 Machi 2024

Magenge ya watu wenye silaha yameanzisha mashambulizi mapya nchini Haiti, na kutokana na hali hiyo Marekani imeanza kuwahamisha raia wake kutoka nchini humo.

https://p.dw.com/p/4dxkT
Haiti, Port-au-Prince, Bandengewalt, gang violence,
Picha: Clarens Siffroy/AFP/Getty Images

Milio ya risasi imesikika katika viunga vilivyo karibu na mji mkuu wa nchi hiyo Port-au-Prince, maeneo ambayo yalikuwa na utulivu.

Wanahabari wa shirika la Habari la Associated Press wameripoti kuiona takriban miili mitano walipozunguka kwenye baadhi ya vitongoji, ingawamagenge ya wababe yameweka vizuizi kwenye baadhi ya maeneo na kuwafanya waandishi hao wa habari kushindwa kufika kwenye maeneo hayo.

Soma Pia:Vikosi vya usalama- vyazima jaribio la kushambulia Benki Kuu ya Haiti

Watu katika maeneo yaliyokumbwa na mashambulizi walipiga simu vituo vya redio wakiomba msaada kutoka kwa jeshi la polisi ambalo lenyewe limesalia na maafisa wachache ambao wanazidiwa nguvu na magenge ya watu wenye silaha wanoudhibiti mji mkuu wa Haiti.

Haiti | Mashambulizi katika mji wa  Port-au-Prince
MACHI 09: Mwanamke akimbilia usalama wake, huku Wahaiti wakilazimika kuyakimbia makazi yao wakati vurugu za magenge zikiongezeka katika mji wa Port-au-Prince,Picha: Guerinault Louis/Anadolu/picture alliance

Kufikia jana Jumatano alasiri, ambapo mashambulizi hayo yalikuwa yakiendelea, Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ilitangaza kwamba ilikuwa imekamilisha zoezi lake la kwanza la kuwahamisha raia wa Marekani kutoka kwenye mji wa Port-au-Prince.

Zaidi ya Wamarekani 15 walisafirishwa kwa ndege hadi katika mji wa Santo Domingo ambao ni mji mkuu wa nchi jirani ya Jamhuri ya Dominika.

Marekani imesema zaidi ya raia wake 30 wataweza kuondoka kutoka kwenye mji wa Port-au-Prince kila siku kwa kutumia ndege za helikopta zilizokodishwa na Idara ya Usimamizi wa Dharura ya Florida.

Soma Pia:Polisi nchini Haiti waendelea kukabiliana na magenge ya wahalifu

Zaidi ya Wamarekani 300 wako nchini Haiti

Gavana wa Florida Ron DeSantis, amesema anaelewa kuwa kuna wamarekani walio hatarini. Gavana huyo wa Florida Ron DeSantis amesema zaidi ya wamarekani 300 kutoka kwenye jiji hilo wako nchini Haiti, na operesheni hiyo ya kuwahamisha inayofadhiliwa na jiji la Florida itaendelea licha ya kukabiliwa na ukiritimba kutoka kwa serikali kuu ya Marekani na pia vitisho vya usalama nchini Haiti.

Maafisa wa Haiti wanajitahidi kufanikisha kuundwa baraza jipya la mpito litakalo kuwa na jukumu la kumteuwaWaziri Mkuu wa mpito na baraza lake la mawaziri.

Chanzo:AP