1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaHaiti

Waziri Mkuu wa Haiti awaomba wananchi kuacha maandamano

Bruce Amani
8 Februari 2024

Waziri Mkuu wa Haiti, Ariel Henry, amehimiza utulivu kufuatia siku tatu za maandamano yenye vurugu ambayo yameathiri shughuli za kawaida nchini humo.

https://p.dw.com/p/4cBaU
Maandamano nchini Haiti.
Maandamano nchini Haiti.Picha: Odelyn Joseph/AP/picture alliance

Waandamanaji wanadai kujiuzulu kwa waziri mkuu. Hotuba yake fupi aliyoitoa leo haijaweza kuwatuliza maelfu ya watu wenye hasira kutokana na kuongezeka kwa machafuko ya megenge, kiwango kikubwa cha umaskini na kutoandaliwa uchaguzi mkuu.

Henry amesema bila kutoa maelezo kuwa anadhani ni wakati sasa kwa kila mmoja kutafakari namna ya kuisaidia Haiti.

Amewahimiza Wahaiti kutoichukulia serikali au Polisi ya taifa kuwa maadui wao.

Matamshi yake yamejiri wakati maelfu ya Wahaiti walikusanyika kila siku wiki hii mijini kote nchini kumtaka Henry ajiuzulu wakisema wataendelea kuandamana hadi asalimu amri.

Polisi jana waliwauwa mawakala watano wa ulinzi wa mazingira waliokuwa na silaha katika mji mkuu Port-au-Prince katika tukio ambalo baadhi wanahofia linaweza kuufanya mzozo wa Haiti kuwa mbaya zaidi.