1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri juu ya Uturuki, Uhispania na Benki Kuu ya Marekani

Abdu Said Mtullya8 Januari 2014

Wahariri wanatoa maoni juu ya Uturuki,Binti wa Mfalme wa Uhispania na juu ya Benki Kuu ya Marekani

https://p.dw.com/p/1Amun
Waziri Mkuu wa Uturuki Tayyip Erdogan
Waziri Mkuu wa Uturuki Tayyip ErdoganPicha: Reuters

Mhariri wa gazeti gazeti la "Die Welt" anasema kuwa ile rangi iliyokuwa inayapamba mafanikio ya nchini Uturuki sasa imeanza kupauka. Hali hiyo inatokana na mvutano baina pande mbili- wa watu fulani mafisadi waliomo katika chama kinachotawala cha AKP na upande unaoongozwa na mhubiri Gülen.

Mhariri huyo anasema wakati mvutano baina ya pande mbili hizo unaendelea, watetetizi wa sera ya kutenganisha dini na siasa wanausubiri mwanya wa kulipiza kisasi.Mhariri wa gazeti la "Die Welt" anasema yote hayo yamesababishwa na ufisadi. Lakini anaepaswa kulaumiwa ni Waziri Mkuu Erdogan alietangaza sera ambazo yeye mwenyewe amezikiuka.

Binti wa Mfalme matatani Uhispania

Gazeti la "Süddeutsche" linatoa maoni juu ya madai yanayomkabili binti wa Mfalme Juan Carlos nchini Uhispania. Binti huyo anakabiliwa na madai ya kukwepa kulipa kodi na kuekeza fedha haramu. Lakini mhariri wa gazeti la "Süddeutsche" anasema familia ya mfalme itafanikiwa kuvihimili vishindo hivyo.

Mhariri huyo anaeleza kuwa tayari mrithi wa mfalme ameshatayarishwa. Mrithi huyo Felipe anazingatiwa kuwa mtu mwerevu na asiyependa makuu.Uchunguzi wa maoni unaonyesha kuwa Felipe ana umaarufu mkubwa nchini Uhsipania.


Benki Kuu ya Marekani.

Mhariri wa gazeti la "Die Rheinpfalz" anazungumzia juu ya kuteuliwa na kuthibitishwa kwa mwanamke wa kwanza Janet Yellen kuwa Mwenyekiti wa Benki Kuu ya Marekani. Mhariri huyo anasema kwamba mama huyo analichukua jukumu nyeti.

Uchumi wa Marekani bado umo katika hali ya mashaka.Licha ya kuitekeleza sera ya riba za chini sana, Benki Kuu ya Marekani bado haijafanikiwa kuurejesha uchumi wa Marekani katika viwango vya ustawi vya hapo awali-yaani kabla ya kufumuka kwa mgogoro mkubwa wa mabenki. Ukosefu wa ajira bado unafikia asilimia 7.

Kwa sasa Marekani ni kama behewa tu, badala ya kuwa injini ya uchumi wa dunia.Nakisi katika bajeti za Marekani ni kama donda dugu. Mfumo wa kuondoa udhibiti wa mabenki sambamba na maamuzi potovu ya wanasiasa, ni mambo yaliyochangia katika kuifanya Benki Kuu ya Marekani iwe na mamlaka ya kupita kiasi katika uchumi wa nchi. Hayo ni matatizo ambayo Mwenyekiti mpya wa Benki hiyo atapaswa kuyashughulikia.

Mwandishi: Mtullya Abdu/Deutsche Zeitungen.

Mhariri: Mohammed Khelef