1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni: Manifesto ya AfD ni hatari kwa Ujerumani

12 Aprili 2021

Chama cha siasa za mrengo wa kulia AfD kinapinga uhamiaji, Umoja wa Ulaya na pia vikwazo vilivyowekwa na serikali kuzuia virusi vya corona kusambaa. Mwandishi wa DW Hans Pfeifer anasema hatua hii ni hatari kwa Ujerumani.

https://p.dw.com/p/3rqxz
Deutschland | AfD Parteitag in Dresden
Picha: Jens Schlueter/AFP/Getty Images

Ikiwa na manifesto yake ya uchaguzi, chama cha AfD kimeanzisha kampeni zake za kuelekea uchaguzi mkuu Ujerumani utakaofanyika kipindi cha mapukutiko mwaka huu wa 2021. Kauli mbiu ya chama hicho ni "Ujerumani, lakini ya kawaida."

Katika kampeni yake, chama hicho kinataka hali ya kawaida kurejea Ujerumani. Katika tangazo lake ambalo imelitoa kupitia ukanda wa video, chama hicho kinaonyesha bibi na babu wenye upendo wakiwakumbatia wajukuu wao, pamoja na familia yenye furaha ikiwa mezani kwa chakula. Video hiyo pia inaonyesha watoto wakiwa na furaha shule.

Kwa mukhtasari, katika ukanda huo wa video, kunaonyeshwa mambo ambayo Wajerumani wanayatamani katika kipindi hiki cha janga la virusi vya corona ambapo serikali imeweka vikwazo vya kuzuia kusambaa kwa virusi hivyo.

Ujumbe wa AfD ni kuibadilisha jamii ya Ujerumani

Video hiyo pia inaonyesha kile ambacho kinatafsiriwa kama maadui wa Ujerumani. Ukanda huo wa video unaonyesha migahawa iliyofungwa baada ya vikwazo vya kuzuia kusambaa kwa virusi vya corona, inaonyesha pia msichana mweupe akiwa akipinga mabadiliko ya tabia nchi pamoja na ujumbe wa maandishi kutoka wa serikali ya Ujerumani kuhusiana na sera yake ya virusi vya corona.

Deutsche Welle Pfeifer Hans Portrait
Mwandishi wa DW Hans PfeiferPicha: DW/B. Geilert

Ujumbe ulioko hasa katika tangazo hili la kampeni za AfD ni mradi mkubwa wa kuibadilisha jamii. Video hiyo bila shaka haionyeshi hilo, ila ni wazi kwamba hilo ndilo lililoamuliwa katika mkutano wa chama hicho mjini Dresden.

Kulingana na manifesto ya chama hicho mtu atatambulika kuwa Mjerumani tu, iwapo ana wazazi ambao ni Wajerumani, kwa hiyo mamia kwa maelfu ya Wajerumani wataachwa nje katika suala la uraia. Chama hicho pia kimeamua, watakaokubaliwa kuhamia Ujerumani ni wale tu ambao watakuwa na zaidi ya yuro milioni tano ili kuuongeza utajiri wa Ujerumani, wasiokuwa na fedha hizo, watafanya kazi Ujerumani kama "wafanyakazi wa kigeni," na watachukuliwa kama raia wa daraja la pili.

AfD huenda kikawa chama chenye nguvu jimbo la Saxony-Anhalt

Chama cha AfD pia kinataka mabadiliko katika sera ya kimataifa, kinataka Ujerumani ijiondoe kutoka kwenye Umoja wa Ulaya na hivyo kufikisha mwisho matumizi ya sarafu ya yuro Ujerumani. Kauli mbiu ya sera yake ya kigeni na usalama ingeweza kuitwa na rais wa zamani wa Marekani Donald Trump, kama, "Ujerumani kwanza."

Ushindi wa CDU na SPD Saxony na Brandenburg wagubikwa na wasiwasi wa AfD kuimarika

Kwa hakika, chama hiki hakiwezi kushinda uchaguzi na kumteua Kansela baada ya uchaguzi ujao na vyama vyengine vyote vya Ujerumani vimetoa hakikisho hilo. Ila chama hiki huenda kikawa chama chenye nguvu zaidi katika jimbo la Saxony-Anhalt na ndio maana manifesto ya chama hiki inastahili kutazamwa kwa makini.

Chama hiki pia hakipendi amani, kinapenda amani tu iwapo amani hiyo si pingamizi katika utekelezaji wa mipango yake na hii ndiyo sababu inayostahili kuwatia hofu Wajerumani.