1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mabaki mapya ya binadamu yavumbuliwa

Josephat Charo9 Agosti 2007

Uvumbuzi wa visukuku vilivyo na umri wa zaidi ya milioni moja unabadili hadithi ya mwanzo wa biandamu. Wanasayansi wanasema uvumbuzi huo unaonyesha kwamba aina mbili za binadamu waliishi pamoja badala ya kufuatana mmoja baada ya mwingine.

https://p.dw.com/p/CHjq

Uvumbuzi wa mabaki ya fizi la binadamu, Homo Habilis, yaliyo na umri wa miaka milioni 1.44 na fuvu la kichwa la binadamu wa sasa, Homo Sapiens, lenye umri wa miaka milioni 1.55, linaupa changamoto mtazamo unaojulikana kwamba binadamu wa kwanza Homo habilis ndiye aliyekua na kugeuka kuwa binadamu wa sasa, homo sapiens. Uvumbuzi huo unapendekeza kwamba aina mbili hizo za binadamu ziliishi pamoja wakati mmoja katika eneo la Afrika Mashariki, kwa zaidi ya miaka nusu milioni.

Wakitangaza juu ya aina mbili za binadamu mjini Nairobi, timu ya wanasayansi wa Kenya walisema wameshangazwa kuona kuwa wanawake wa kwanza walikuwa wadogo kuliko wanaume. Fuvu la kichwa lililogunduliwa ni la kwanza la binadamu wa kike aina ya homo erectus.

Kabla uvumbuzi huo wanasayansi hawakujua kwamba binadamu wa kikume aina ya homo erectus walikuwa wakubwa zaidi kuliko wa kike, alisema Dr Emma Mbua, mmoja wa wataalamu waliotoa taarifa hiyo katika jumba la makumbusho la kitaifa mjini Nairobi. Alisema kujamiiana kati ya binadamu hao inachukuliwa kuwa tabia ya zamani kwa sababu ilidhihirika pia miongoni mwa sokwe wengine.

Dr Emma aliongeza kusema hii inaweza kuwa na maana kwamba tabia ya aina ya binadamu, homo erectus, ya kufanya mapenzi ilifanana na ile ya sokwe, ambapo wanawake lakini sana wanaume, walijamiiana na wapenzi mbalimbali, mara nyengine kwa saa kadhaa, ikilingansishwa na aina ya binadamu waliotangulia.

´Binadamu wa kwanza, Homo habilis, hakusababisha kuchipuka kwa aina ya pili ya binadamu, homo sapiens. Kwa muda mrefu tumekuwa tukiamini hivyo lakini sasa kugunduliwa kwa mabaki haya mapya kunabadili kabisa historia hiyo,´ alisema Frederick Manthi, mwanasayansi aliyevumbua mabaki hayo mashariki mwa ziwa Turkana, kaskazini mwa Kenya mnamo mwezi Agosti mwaka wa 2000.

Bwana Manthi ameeleza mabadiliko hayo mapya katika historia ya binadamu kwamba alifanana na nyani na sokwe walioishi wakati mmoja lakini katika mazingira tofauti. Hiyo ina maana hawakuwa katika mashindano ya kupigania mahitaji ya kuwawezesha kuendelea kuishi.

Idle Farah, mkurugenzi wa jumba la makumbusho la kitaifa mjini Nairobi, Kenya, amesema ukweli kwamba waliishi mbalimbali kama aina fulani ya binadamu kwa muda mrefu, unapendekeza walikuwa na makaazi tofauti na kujiepusha na mashindano. Taasisi hiyo ilishiriki katika uvumbuzi huo mpya wa mabaki ya binadamu pamoja na mradi wa utafiti wa Koobi Fora ulioongozwa na wanasayansi, Meave na Louise Leakey.

Mawazo ambayo yamekuwepo yanapendekeza kwamba binadamu wa kwanza, homo erectus, aliyeishi kati ya miaka milioni 1.7 na laki mbili iliyopita, aligeuka kuwa aina nyengine ya binadamu, homo habilis, aliyeishi kati ya miaka milioni mbili na milioni 1.6 iliyopita.

Nadharia hiyo mpya ilichapishwa jana tarehe tisa mwezi Agosti katika toleo la jarida la maswala ya sayansi liitwalo, Nature.