1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wajerumani hawaridhishwi na serikali ya Kansela Merz

Amina Abubakar dpa/reuters
24 Novemba 2025

Ripoti iliyotolewa na taasisi ya utafiti wa maoni ya INSA kwa niaba ya gazeti mashuhuri la Bild la hapa Ujerumani, imeonyesha kuwa wajerumani hawaridhishwi na serikali iliyoko madarakani.

https://p.dw.com/p/544RT
Deutschland  2025 | Friedrich Merz
Utafiti waonyesha wajerumani hawaridhishwi na serikali ya muungano ya Kansela Friedrich Merz Picha: dts-Agentur/picture alliance

Asilimia 22 pekee ya waliohojiwa ndio wanaoridhishwa na serikali ya muungano inayoongozwa na kansela Friedrich Merz, ikiwa chini kwa nukta mbili ikilinganishwa na utafiti uliofanyika Novemba 7.

Asilimia 67 bado hawajaridhishwa na serikali ya Merz huku asilimia 11 ikikataa kutoa maoni.

Taasisi hiyo iliwahoji watu 1,004 kati ya Novemba 20 na 21 na iliwauliza iwapo wanaridhia kazi ya Merz kama Kansela na iwapo pia wanaridhishwa au kutoridhishwa na serikali yake.Asilimia 25 ilipitisha na kuipenda kazi ya Merz, asilimia 64 haijaridhika nayo huku asilimia 11 ikikataa kutoa maoni.

Haya yanajiri wakati Merz mwezi uliopita alikabiliwa na ukosoaji mkubwa kutoka kwa wabunge wa upinzani, juu ya kauli yake ya kufukuzwa kwa wahamiaji yaliyotafsiriwa kuwa ya kibaguzi. Merz alitoa kauli hiyo wakati akijibu suali  kuhusu ushawishi wa chama cha siasa kali AfD na juhudi za serikali yake kurekebisha sera ya uhamiaji.

Steinmeier: Itikadi kali za mrengo wa kulia ni kitisho kwa demokrasia

Ripoti ya INSA imetolewa wakati hivi karibuni rais wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier alionya kuwa ongezeko la itikadi kali za mrengo wa kulia na ubaguzi dhidi ya wayahudi vinazidi kutishia demokrasia nchini humo.

Steinmeier alizungumzia kuhusu ongezeko la siasa kali za mrengo wa kulia katika mfumo wa chama kinachopinga wahamiaji  cha Alternative for Germany (AfD), ambacho kilipata asilimia 20.5 ya kura katika uchaguzi mkuu wa Februari na kushika nafasi ya pili.