1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yakaza sheria dhidi ya COVID-19

Lilian Mtono
1 Agosti 2021

Wasafiri wanaoingia Ujerumani kutokea nchi nyingine hivi sasa watatakiwa kuwasilisha vipimo vinavyoonyesha hawana maambukizi ya virusi vya corona, vinginevyo wawe wamechanjwa dozi kamili ama wamepona maradhi ya COVID-19.

https://p.dw.com/p/3yNxV
Deutschland | Coronavirus | Restaurantbesuch in Düsseldorf
Picha: Ying Tang/NurPhoto/picture alliance

Wasafiri wanaoingia nchini Ujerumani kutokea nchi nyingine hivi sasa watatakiwa kuwasilisha vipimo vinavyoonyesha hawana maambukizi ya virusi vya corona, vinginevyo wawe wamechanjwa dozi kamili ama wamepona maradhi ya COVID-19.

Kanuni hizi mpya zinazoanza kutumika Jumapili hii ya Agosti Mosi, zinatangazwa wakati kukiongezeka wasiwasi kuhusiana na kudhibiti kusambaa kwa kirusi aina ya Delta na maafisa wakihofu kuhusu maambukizi zaidi kutoka kwa wasafiri walioenda likizo nje ya Ujerumani.

Kanuni mpya ni zipi?

Chini ya kanuni mpya watu kuanzia miaka 12 na ambao hawajachanjwa watatakiwa kupima.

Watu walioachanjwa na wale waliopona maradhi ya COVID-19 hawatalazimika kupima, lakini watalazimika kuonyesha nyaraka zinazothibitisha kwamba wamepata dozi kamili ya chanjo ama kupona.

Einreise EU | Covid-19: Airport Corona Testing
Afisa wa Ujerumani akithibitisha vipimo vya corona vya msafiri anayeingia nchini humo.Picha: Zumapress/picture alliance

Wasafiri wanaopitia Ujerumani kuelekea maeneo mengine na wanaovuka mipaka hawataguswa na kanuni hizo mpya.

Vipimo vya haraka havitachukuliwa masaa 48 kabla ya kuingia Ujerumani, lakini kipimo cha CPR kitachukuliwa katika kipindi kisichozidi masaa 72. Kwa wale wanaoingia kutoka kwenye maeneo yenye maambukizi makubwa ya kirusi cha Delta, kipimo cha haraka kitakachokubalika ni kile kisichozidi masaa 24.

Nini kimebadilika?

Kabla ya mabadiliko haya, wasafiri waliokuwa wakiingia Ujerumani walitakiwa kuonyesha vipimo vinavyoonyesha hawana maambukizi ama uthibitisho wa chanjo ama iwapo walipona maambukizi. Sasa kanuni hizi zitawahusu wale wanaoingia Ujerumani kwa njia ya gari, treni ama meli.

Deutschland Euskirchen | Nach dem Unwetter | Horst Seehofer
Picha: Roberto Pfeil/dpa/picture alliance

Mafisa wa Ujerumani wanasemaje?

Waziri wa mambo ya ndani wa Ujerumani Horst Seehofer amesema kutakuwepo na upimaji endelevu, huku akionya adhabu kali kwa wale watakaokiuka kanuni hizi mpya.

Soma Zaidi: Maelfu waandamana Ulaya kupinga vizuizi vya Covid-19

"Yoyote anayeingia Ujerumani analazimika kujiandaa kupimwa", ameliambia gazeti la Jumapili la hapa Ujerumani la Bild am Sonntag.

Kutakuwepo na upimaji wa hapa na pale kwenye njia kuu za mipakani ili kuzuia msururu wa watu wanaosafiri kwenda likizo.

"Yoyote atakayekutwa na maambukizi atapaswa kukaa karantini. Na watu wote wanaoingia Ujerumani kutoka mataifa ambayo si wanachama wa Umoja wa Ulaya na wanaoingia kwa ndege ama njia ya bahari watapimwa," ameongeza Seehofer.

Deutschland | Coronavirus  Covid-19-Dashboard RKI 7-Tage-Inzidenz 9,4
Picha: Rüdiger Wölk/imago images

Kiwango cha maambukizi Ujerumani, kikoje?

Nchini Ujerumani, utoaji wa chanjo unazidi kuongezeka baada ya kuanza taratibu sana. Zaidi ya asilimia 61 ya Wajerumani wamepata dozi ya kwanza ya chanjo dhidi ya COVID-19. Zaidi ya asilimia 51 tayari wamepata dozi kamili.

Katika hatua nyingine, taasisi ya kupambana na magonjwa ya kuambukiza nchini Ujerumani ya Robert Koch imearifu kwamba visa vya maambukizi vinazidi kuongezeka, wakati Jumapili hii ikirekodi visa 2,097, vikiwa ni 710 zaidi ya vilivyorekodiwa Jumapili iliyopita.

Hata hivyo idadi hiyo ni ndogo ikilinganishwa na mataifa jirani kamaUfaransa, Uhispania na Uholanzi.

Soma Zaidi: Ujerumani: Viongozi wataka hatua zote za karantini ziondoshwe

Mashirika: DW