1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Macron aupongeza ushirikiano wa Ufaransa na Ujerumani

27 Mei 2024

Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa ameupongeza ushirikiano wa muda mrefu wa nchi yake na Ujerumani, wakati akianza ziara yake ya kiserikali ya siku tatu mjini Berlin inayolenga kudhihirisha nguvu ya uhusiano huo.

https://p.dw.com/p/4gJGE
Macron ziarani Ujerumani
Rais Macron wa Ufaransa yuko katika ziara ya kiserikali ya siku tatu nchini UjerumaniPicha: Liesa Johannssen/REUTERS

Ziara ya kiserikali ya Macron nchini Ujerumani, ya kwanza kufanywa na rais wa Ufaransa katika miaka 24, inajiri wakati madola hayo mawili makubwa Ulaya yanakabiliwa na matatizo mbalimbali, kuanzia vita vinavyorindima kwenye mlango wa Umoja wa Ulaya nchini Ukraine mpaka kuongezeka kwa vyama vya siasa kali za mrengo wa kulia katika umoja huo na uwezekano wa kurejea madarakani Donald Trump mjini Washington.

Macron amesema Ulaya ipo katika wakati muhimu wa maamuzi, akitaja uvamizi wa kijeshi wa Urusi pamoja na changamoto zinazohusiana na mabadiliko ya tabianchi na akili ya kubuni - AI.

Amesema ili kuyashughulikia masuala hayo, ushirikiano kati ya Ufaransa na Ujerumani unahitajika. Katika kikao cha waandishi habari pamoja na Rais wa Ujerumani Frank Walter-Steinmeier katika ikulu ya Bellevue mjini Berlin, Macron alisema ushirikiano kati ya Ujerumani na Ufaransa ni kama wanandoa wachangamfu, wenye masharti na malengo makubwa.

Macron ziarani Berlin
Macron na Steinmeier walisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa Ufaransa na Ujerumani wakati wa ziara hiyoPicha: Christian Mang/REUTERS

Steinmeier ameiitaziara ya Macronkuwa ni uthibitisho wa ukubwa wa urafiki kati ya Ufaransa na Ujerumani. Macron aliwasili jana Berlin na akashiriki Tamasha la Demokrasia lililoadhimisha miaka 75 ya katiba ya Ujerumani iliyoanza kutumika katika Iliyokuwa Ujerumani ya Magharibi baada ya Vita vya Pili Vikuu vya Dunia.

Kisha baadae akaandaliwa dhifa ya chakula cha jioni iliyohuhudhuriwa na wanasiasa wakuu, akiwemo Kansela Olaf Scholz.

Ziara ya Macron imejiri kabla ya uchaguzi wa Ulaya utakaoamua Bunge lijalo la Ulaya. Vyama vya siasa kali za mrengo wa kulia katika Umoja wa Ulaya vimehuhudia ongezeko la uungwaji mkono katika miaka ya karibuni – ikiwemo Ufaransa na Ujerumani – na vinatarajiwa kufanya vyema katika uchaguzi huo wa Juni 6 – 9.

Soma pia: Rais Macron kufanya ziara rasmi Ujerumani Mei 26

Uhusiano kati ya Paris na Berlin kwa muda mrefu umeonekana kuwa nguvu inayoendesha Ulaya, kisiasa na kiuchumi. Lakini msuguano ulianza kuzuka 2022, baada ya Angela Merkel kuondoka jukwaa la kisiasa la Ujerumani, ijapokuwa Macron na Scholz katiku ziku za karibuni wamefanya juhudi za kuimarisha ushirikiano.

Makubaliano yamepatikana kuhusu masuala kadhaa, ikiwemo mageuzi ya sheria za Umoja wa Ulaya za madeni na nakisi, lakini mambo mengine ya mgongano bado yapo, hasa kiwango cha msaada wa kijeshi kwa Ukraine na majibu ya kiuchumi ya Umoja wa Ulaya kwa hatua za ulinzi wa masoko za China na Marekani. Maswali hayo nyeti na mengine yanatarajiwa kujadiliwa katika mkutano wa mawaziri wa Ufaransa na Ujerumani Jumanne. Jumatatu Macron na mkewe watakwenda Dresden. Atatoa hotuba kuhusu sera ya Ulaya.

Jumanne, watakuwa mjini Münster, ambako Macron atapewa Tuzo ya Amani ya Westphalia. Macron aliingia madarakani Ufaransa miaka saba iliyopita na hawezi kugombea kwa muhula wa tatu katika uchaguzi ujao wa rais mwaka wa 2027.

Macron ashinda awamu ya pili ya urais

dpa