1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maandamano dhidi ya mrengo mkali wa kulia yaenea vijijini

Peter Hille | Iddi Ssessanga
26 Januari 2024

Kumekuwa na maandamano ya nchi nzima dhidi ya chama cha siasa kali za mrengo wa kulia, AFD. Mwandishi wa DW Peter Hille alitembelea kijiji kidogo ambako wawakilishi wa AfD na wapinzani wao walikabiliana.

https://p.dw.com/p/4bjUK
Tukio la Eitorf | AfD na maandamano ya kuwapinga
Mjini Eitorf, polisi walikuwa wakiwatenganisha wafuasi wa chama cha siasa kali za mrengo wa kulia cha AfD, na maandamano ya kukabiliana nao.Picha: Peter Hille/DW

Kituo cha kijamii katika mji wa Eitorf magharibi mwa Ujerumani kilikuwa eneo la makabiliano kati ya chama cha siasa kali za mrengo wa kulia cha Alternative for Germany (AfD) na wapinzani wake wiki hii: Mbunge wa AfD na wafuasi wake walikabiliana na waandamanaji wanaohofia kwamba ufashisti unarudi tena.

Ayfer Evmez alishudia kila kitu kutokea dirisha la ofisi yake. Alikuwa ameandaa keki na vyakula vingine kwa ajili waandamanaji. Evmez anaendesha huduma ya utunzaji kwa wazee na wagonjwa huko Eitorf. Alikuja Ujerumani akiwa mtoto mchanga; sasa ana umri wa miaka 48 na ana wafanyakazi 60 kutoka zaidi ya mataifa kadhaa.

Jioni hiyo, wabunge wa AfD na wafuasi kadhaa walizungumza kuhusu kile wanachoita "uhamiaji," kuwafukuza mamilioni ya watu wenye asili ya wahamiaji kutoka Ujerumani. Evmez anaiona dhana hiyo kuwa ya kusikitisha - na haina maana. "Tayari tuna matatizo ya kupata wafanyakazi. Na watu wengi tulio nao wana asili ya uhamiaji. Kama wote wataondoka, mfumo mzima utaanguka. Hilo siyo jambo zuri kwa nchi yetu," alisema.

Tukio la Eitorf  | AfD na maandamano ya kuwapinga
Ayfer Evmez (kulia) na wafanyakazi wenzake walikuwa wametayarisha keki na kahawa kwa ajili ya waandamanaji wanaopinga siasa kali za mrengo wa kulia.Picha: Peter Hille/DW

Maandamano ya vyama mbalimbali

Evmez alifurahi kuona umati unaoongezeka wa waandamanaji wanaopinga siasa kali za mrengo wa kulia nje ya dirisha lake jioni hiyo. Walikuwa wamebeba nyuzi za rangi za taa au bendera kutoka makundi ya mrengo wa kushoto na vyama vyote vya kisiasa ikiwa ni pamoja na chama cha kihafidhina cha Christian Democratic Union, CDU.

Soma pia: Hofu ya "fashisti" kuongoza serikali ya jimbo Ujerumani

Lakini hakuna hata mmoja wao aliyefanikiwa kuja na kuonja keki alizowaandalia, kwa sababu kundi la wafuasi wapatao kumi wa AfD waliweka kambi nje ya dirisha lake, wakiwa wamebeba bango. Mbele yao kulikuwa na safu ya maafisa wa polisi waliovalia kofia, kudhibiti watu.

Mwanamume mwenye ndevu aliekuwa anapeperusha bendera nyeusi alisema alikuwa ametoka katika eneo la mashambani ambako mrengo makli wa kulia una nguvu. "Tunataka kutuma ishara ya wazi dhidi ya AfD," alisema. Alikuwa akiandamana dhidi ya watu wenye itikadi kali za mrengo wa kulia katika miaka ya 1990 walipokuwa wakipata nguvu. "Hili sio jambo geni kwangu," alisema. "Lakini sasa nina hisia kwamba hata watu wa tabaka la kati walioridhika wanatambua kwamba wanapaswa kusimama."

Alexander Leistner, mwanasayansi wa siasa katika Chuo Kikuu cha Leipzig, anathibitisha maoni haya. Katika mahojiano kwa njia ya simu, aliiambia DW kwamba mafanikio ya AfD katika chunguzi za maoni yamewatia wasiwasi watu wengi.

Wakati jukwaa la vyombo vya habari la Correctiv lilipochapisha ripoti ya uchunguzi juu ya mkutano wa siri wa wanasiasa wa AfD na watu wenye msimamo mkali wa mrengo wa kulia katika jumba la kifahari karibu na Potsdam, kujadili mipango ya kufukuzwa kwa mamilioni ya watu kutoka Ujerumani watu wengi waliamka na kujua ukweli. "Hiyo ilivuka mstari. Watu wengi waligundua kwamba walipaswa kusema, 'Tunafikiri hii ni hatari,'" Leistner alisema.

Tukio la Eitorf | AfD na maandamano ya kuwapinga
Christa Kurtidis ameishi Eitorf maisha yake yote na amejiunga na kikundi cha 'Grannies against the far right' (Mabibi dhidi ya mrengo mkali wa kulia).Picha: Peter Hille/DW

Maandamano hayo hapo awali yalifanyika hasa katika miji mikubwa, lakini sasa, mwanasayansi wa siasa Leistner alisema, yamechuja hadi katika miji midogo na jumuiya. "Waandamanaji ni pamoja na familia na wazee. Wengine wanasema kwamba wamekuwa wakifanya maandamano kwa miaka mingi, wengine hawajawahi kufanya hivyo hapo awali," alisema.

Soma pia: Serikali ya Ujerumani yakabiliwa na mwaka mgumu mbele yake

Leistner anatarajia maandamano yataisha wakati fulani. "Lakini miungano mipya inaibuka, hasa katika majimbo ambayo uchaguzi unakuja, ikiwa ni pamoja na Thuringia." Anataja vuguvugu la mashinani la "Grannies Against the Right", ambao mara nyingi hufanya harakati zake katika miji midogo zaidi.

Mmoja wao ni Christa Kurtidis mwenye umri wa miaka 63 ambaye ameishi Eitorf kwa miongo mitano. "Nina hofu kwamba familia yangu italazimika kuondoka ikiwa AfD itaingia madarakani. Sisi ni raia wa nchi mbili za Ugiriki na Ujerumani. Hatukuzaliwa hapa. Hilo linanitia kichefuchefu. Sina marafiki wala jamaa nchini Ugiriki. Eitorf ni nyumbani kwangu," alisema.

Takriban waandamanaji 3,000 walishiriki katika maandamano ya Eitorf jioni hiyo, wakihimili mvua na baridi kali. Meya Rainer Viehof, ambaye hafungamani na chama chochote, alikuwepo pia. Aliiambia DW kuwa alitoa kibali kwa tukio la AfD katika kituo cha jumuiya kwa kuzingatia kanuni ya usawa kwa vyama vya siasa. Lakini aliongeza, "Kama meya, nina furaha kwamba Eitorf inasimama na kupinga jambo hili waziwazi. Nina furaha kwamba watu hawa wote wamekuja kutoa sauti zao dhidi ya ufashisti na dhidi ya AfD."

Tukio la Eitorf | AfD na maandamano ya kuwapinga
Mwanasiasa wa AfD Roger Beckamp alijaribu kuwahutubia waandamanaji wanaoipinga AfDPicha: Peter Hille/DW

AfD yajitetea

Mwanasiasa wa AfD Roger Beckamp ni mwakilishi wa Eitorf katika bunge la shirikisho. Alijaribu kuwahutubia waandamanaji wanaoipinga AfD lakini akanyamazishwa na umati wa watu.

Ndani ya kituo cha jamii, Beckamp aliiambia DW kuwa chama chake ni mwathirika wa vyombo vya habari vilivyoanzishwa." Ghadhabu hii ya vyombo vya habari tuliyonayo hivi sasa juu ya kisa cha Potsdam imepangwa," alisema na kuendelea: "Sio nzuri, kwa sababu inawasilishwa kwa njia potofu na vyombo vyote vya habari vinairukia."

Soma pia: Kongamano la AfD kuweka mikakati zaidi ya ushindi mwakani

Alizitaja ripoti kwamba AfD inataka kuwafukuza mamilioni ya raia wa Ujerumani wenye asili ya wahamiaji "upuuzi mtupu. Hakuna aliyewahi kusema hivyo." Hata hivyo, ripoti ya Correctiv imefanya neno "uhamiaji" kuwa sehemu ya mjadala wa umma - jamboa amablo AfD inaliona kama ushindi. "Hatungeweza kamwe kufaulu kuiingiza katika ufahamu wa umma kama vile kampeni hii ya vyombo vya habari imefanya," Beckamp alisema.

Je, uhamiaji ni tishio kwa Ujerumani?

Wakati wafuasi wa AfD na waandamanaji waliposonga mbele kutoka dirishani kwake, Ayfer Evmez alishusha pumzi ndefu. "Hiyo ilikuwa ya kutisha," alisema, lakini pia aliona ni vyema waandamanaji walikuwa na sauti kubwa kiasi kwamba AfD haikuweza kueleza ujumbe wake.

Wakati huo huo, wafanyakazi wauguzi wa kampuni yake wenye asili tofauti wamekuwa wakifanya kazi, wakiendesha gari kote nchini kuhudumia watu. "Tuko kwenye zamu ya jioni. Watu wanapaswa kulazwa jioni, wagonjwa wa kisukari wanapaswa kupata sindano zao za insulini, "Evmez alielezea, na kuongeza kuwa anashukuru kwa kila mfanyakazi wake, bila kujali wanatoka wapi.