Kesi ya Mubarak yafunguliwa Cairo
3 Agosti 2011Hii ni mara ya kwanza kwa Mubarak kutokeza hadharani tangu alipopinduliwa mwezi wa Februari 11 kufuatia maandamano makubwa yaliyoibuka nchini humo Janauari 25. Mubarak alie na umri wa miaka 83 amepelekwa mahakamani akiwa amejinyosha kwenye kitanda cha hospitali na akaingizwa kizimbani pamoja na wanae Alaa na Gamal. Mubarak ameletwa kutoka mji wa mapumziko wa Sharm el Sheikh ambako alikuwa kizuizini kwenye hospitali moja akipokea matabu ya ugonjwa wa moyo. Hapo awali, wakili wake Farid al-Deeb alisema, afya ya Mubarak haimruhusu kufikishwa mahakamani. Lakini jeshi lililoshika madaraka baada ya Mubarak kujiuzulu, limeazimia kuonyesha kuwa sio tiifu tena kwa kiongozi huyo wa zamani.
Waziri wa ndani wa zamani Habib al-Adly na maafisa sita wa polisi vile vile wamefikishwa mahakamani. Mubarak alimtegemea waziri wake huyo wa ndani, kuzima uasi uliomtimua madarakani. Washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka ya kupora mamilioni ya dola kutoka hazina ya serikali na pia kutoa amri ya kuwaua waandamanaji waliokuwa wakipinga utawala wa Mubarak.
Mahakamani, Mubarak atakabiliana na jamaa na ndugu wa watu waliouliwa wakati wa maandamano, ikidaiwa kuwa amri hiyo ilitoka kwa Mubarak. Hadi alipojiuzulu Februari 11, zaidi ya watu 850 waliuawa wakati wa maandamano hayo ya upinzani.
Hii leo, zaidi ya polisi elfu moja wa kuzuia ghasia wanalinda lango la kuingilia jengo la Chuo cha Polisi lililozingirwa na uzio. Ghasia zilizuka nje ya jengo hilo baada ya wafuasi wa Mubarak na wapinzani wake kurushiana mawe. Polisi wakaingilia kati kuzuia mapambano hayo.
Mubarak mwenye miaka 83, ni kiongozi wa pili wa Kiarabu kutimuliwa madarakani katika ghasia zilizozuka Afrika ya Kaskazini na Mashariki ya Kati mapema mwaka huu. Makundi ya kimataifa ya haki za binadamu yametoa mwito wa kufanywa kesi ya haki na iliyo wazi.
Mwandishi: Martin,Prema/afpe,dpae
Mhariri:Abdul-Rahman