1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kenya itahakikisha makubaliano ya kugawana madaraka yafanikiwa

8 Machi 2008
https://p.dw.com/p/DL0A

BERLIN:

Kenya inadhamiria kuhakikisha kuwa makubaliano ya kugawana madaraka yaliotiwa saini kwa azma ya kumaliza mgogoro wa kisiasa nchini humo yatafanikiwa.Hayo alitamka Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya Moses Wetangula baada ya mazungumzo yake pamoja na waziri mwenzake wa Ujerumani Frank Walter Steinmeier mjini Berlin.Waziri Wetangula alikuwa katika ujumbe wa Kenya uliohudhuria maonyesho ya kitaifa ya utalii-ITB mjini Berlin katika juhudi ya kuihakikishia sekta ya utalii kuwa Kenya inarejea katika hali ya utulivu wa kisiasa.

Kenya ilishuhudia umwagaji mkubwa wa damu kufuatia uchaguzi wa Desemba 27 uliomrejesha madarakani Rais Mwai Kibaki.Kiongozi wa upinzani Raila Odinga ametuhumu kuwa uchaguzi huo ulifanyiwa hila.Pande hizo mbili hasimu zilitia saini makubaliano ya kugawana madaraka Februari 28 baada ya kuwa na majadiliano marefu chini ya uongozi wa Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa Kofi Annan.