Kansela Merkel leo akamalisha ziara yake nchini Uturuki
30 Machi 2010Kansela Merkel amesema Ujerumani ipo tayari kusaidia mradi huo. Ni matumaini ya Ujerumani na Uturuki kuwa chuo kikuu cha pamoja kinachotazamiwa kujengwa Istanbul kitaimarisha ushirikiano kati ya nchi hizo mbili. Alipozungumza na wanafunzi wa shule ya Kijerumani mjini Istanbul, Merkel alisema mradi huo ulikuwa ukishughulikiwa tangu muda mrefu.
Hata Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki Ahmet Davutoglu aliesoma katika shule ya Kijerumani mjini Istanbul amesifu pendekezo la kujenga chuo kikuu hicho cha pamoja. Akisifu mchango unaotolewa na shule inayosomesha kwa lugha ya kigeni,amesema, shule hiyo ni daraja linalounganisha nchi mbili na amesisitiza umuhimu wa shule hiyo katika mfumo wa elimu nchini Uturuki.
Kwa upande mwingine,Kansela Merkel akiendelea na siku ya pili ya ziara yake nchini Uturuki, ametembelea Kanisa la Hagia Sophia,lililojengwa karne ya sita na kufanywa msikiti katika mwaka 1453 na hatimae katika mwaka 1935 kuwa jumba la makumbusho linalovutia watalii kutoka kila pembe ya dunia. Merkel vile vile ametembelea msikiti ulio maarufu kama "Msikiti Buluu." Mji wa Istanbul sawa na mji wa Ujerumani wa Essen ni mji mkuu wa utamaduni mwaka 2010.
Lakini bado kuna tofauti ya maoni kati ya Kansela wa Ujerumani Merkel na Waziri Mkuu wa Uturuki Tayyip Erdogan hasa katika suala la uanachama wa Uturuki katika Umoja wa Ulaya. Merkel anapendekeza ushirikiano wa aina ya pekee badala ya uanachama kamili, jambo linalopingwa kabisa na Ankara. Viongozi hao wameshindwa pia kuafikiana katika masuala mengine yenye utata kama kujumuishwa kwa Waturuki wanaoishi nchini Ujerumani na kuiwekea Iran vikwazo vipya katika mgogoro unaohusika na mradi wake wa nyuklia.
Baadae leo hii Kansela Merkel na Waziri Mkuu Erdogan watahudhuria mkutano wa wafanya biashara wa Ujerumani na Uturuki. Ujerumani ni mmoja wa washirika muhimu wa Uturuki katika sekta ya biashara. Merkel anatazamia kurejea nyumbani leo usiku.
Mwandishi: Martin,Prema/DPA
Mhariri: Hamidou,Oummilkheir