1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahariri wa magazeti wamshutumu Donald Trump

Zainab Aziz
17 Agosti 2017

Katika kurasa zao za maoni wahariri wa magezi kadhaa wamemshutumu rais wa Marekani Donald Trump kwa kuugeuza msimamo wake juu ya makundi ya siasa kali za mrengo wa kulia.walioshiriki vurugu za Charllotensville.

https://p.dw.com/p/2iObV
USA Präsident Donald Trump PK im Trump Tower in New York
Picha: picture-alliance/newscom/UPI Photo/J. Angelillo

Hapo awali rais Trump aliwalaani watu hao yaani Manazi mambo leo na wale wanaoamini kwamba watu weupe ni bora kuliko binadamu wengine.  Juu ya ugeugeu wa rais Trump mhariri wa gazeti la Neue Osnabrücker anasema Trump anajifungamanisha na Mafashisti mambo leo na wabaguzi wa rangi wa kundi la KU-Klux Klan, KKK.

Mhariri wa gazeti hilo la Neue Osnabrücker anasema Trump anajishikamanisha na watu hao kwa sababu hataki kueleza kile ambacho makundi hayo yanakiwakilisha yaani chuki dhidi ya Wayahudi na wendawazimu wa ubaguzi wa rangi.  Mhariri wa gazeti hilo anatahadharisha kwamba Trump anajenga mazingira yatakayochochea ghasia na chuki dhidi ya jamii za wachache nchini Marekani. Naye mhariri wa gazeti la Frankfurter Rundschau anasikitishwa na msimamo wa Trump na anasema:

Rais Trump ni mbumbumbu mkubwa anayeamini kwamba wapo wazuri miongoni mwa Manazi mamboleo wanaotoa kauli kwa sauti kubwa za chuki dhidi ya Wayahudi. Msimamo wa rais Trump wa kuyatetea makundi yenye itikadi kali za kibaguzi unaonyesha kwamba rais amepoteza dira ya maadili ndiyo sababu lazima aondolewe haraka madarakani.

Hata hivyo gazeti la Die Tageszeitung linasema litakuwa jambo la kipumbavu kutaraji Trump atayalaani makundi yenye siasa kali za mrengo wa kulia.  Gazeti la Frankfurter Rundschau pia linazungumzia juu ya mwito wa waziri wa maswala ya kijamii Katarina Barley wa kutaka iwekwe idadi maalumu ya akina mama kwenye bodi za uongozi.  Mhariri wa gazeti hilo anaelezea:

Sera ya kuweka idadi maalumu ya wanawake katika sehemu za uongozi kimsingi ni upuuzi.  Utaratibu huo unaashiria kwamba wanawake hawana uwezo wala dhamira ya kuyatekeleza majukumu bila ya kusaidiwa. Ila tu watetezi wa haki za wanawake wanatumia muda mwingi kulalamika juu ya mambo ya kipuuzi badala ya kuweka mkazo juu ya mambo muhimu kama vile kushiriki kikamilifu katika uongozi, kwenye sekta ya uchumi sambamba na kuendesha harakati za haki za kudai mishahara sawa. Lakini inafaa kutilia maanani Ujerumani bado ni nchi ya kina baba, hilo kwa kweli sio jambo zuri kwa jamii kwa sababu wanawake na wanaume kwa pamoja wanafanya kazi nzuri kwa hiyo pana haja ya kuuweka utaratibu huo wa idadi maalumu ya wanawake katika uongozi.

Mwandishi: Zainab Aziz/Neue Osnabrücker Zeitung/Die Tageszeitung/Frankfurter Rundschau

Mhariri:Josephat Charo