1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump aitumia Israel kutia mafuta katika moto

Sekione Kitojo
16 Agosti 2019

Hatua ya Rais Trump kuhimiza na kuunga mkono uamuzi wa Israel kuwazuia wabunge wa chama cha Democratic kuitembelea nchi hiyo huenda ikawa vizuri kwa ngome yake kisiasa, lakini ni hatari kwa uhusiano wa nchi hizo.

https://p.dw.com/p/3NzdE
Ilhan Omar und Rashida Tlaib
Picha: picture-alliance/AP Photo/J. S. Applewhite

Hatua  hiyo  ya  kuwazuwia  wabunge Rashida Tlaib  wa  jimbo  la Michigan  na Ilhan Omar wa  jimbo  la  Minnesota kuingia  Israel imechochea  moto wa mpambano na  chama  hicho kuelekea  taifa hilo  la  Kiyahudi  ambao  umekuwa  ukiendelea  kuwaka  nchini Marekani, huku  Trump akiupulizia kwa  nguvu  moto  huo.

Trump amesherehekea  na  uamuzi  wa  Israel katika  ukurasa  wa Twitter  na ameliweka suala  hilo  mahususi  katika  muktadha wa kisiasa: "Wawakilishi Omar  na  Tlaib ni sura ya  chama  cha Democratic, na wanaichukia Israel! " ameandika  Trump.

Muda  mfupi  kabla  ya  uamuzi  huo  kutangazwa, Trump  alitoa ishara ya kumzindua  waziri  mkuu  wa Israel Benjamin Netanyahu, akiandika  katika  ukurasa wa  Twitter kwamba " Itakuwa  kuonesha udhaifu  wa  hali ya juu " iwapo Israel  itawaruhusu wanawake  hao kufanya ziara nchini  humo. 

"Nahusika tu na msimamo kwamba wanawapinga Wayahudi na wanaipinga Israel. Nafikiri mambo waliyosema ni ya kuchukiza. Mna orodha, hili sio kosa la kwanza. Kile walichosema kuhusu Israel na  Wayahudi  ni kitu kibaya sana na wamekuwa taswira ya chama cha Democratic."

Faida za kisiasa kuelekea uchaguzi

USA l US-Präsident Donald Trump - Oval Office - wütend
Rais wa Marekani Donald TrumpPicha: Getty Images/AFP/N. Kamm

Uungaji  mkono kutoka  vyama  vyote  katika  bunge  la  Marekani Congress umekuwa  msingi  wa  uhusiano  baina  ya  Israel  na Marekani tangu  kuundwa  kwa  taifa  hilo la Kiyahudi, na  wakosoaji  wa uamuzi  wa  jana Alhamis wamesema  wana  hofu  kwamba  Trump na  Netanyahu  wanatumia  hali  hiyo kwa  ajili  na  faida  ya kisiasa ya muda  mfupi.

Netanyahu  anakabiliwa  na  uchaguzi  mwezi  ujao, na  Trump anakabiliwa  na uchaguzi mwakani.

Tlaib na  Omar , wabunge  wawili waliochaguliwa  hivi  karibuni ambao  ni  waislamu , ni  wakosoaji  wa  jinsi  Israel  inavyowafanyia Wapalestina. Walipanga  kufanya  ziara  mjini  Jerusalem  na  Ukingo wa  Magharibi  katika  ziara  iliyotayarishwa  na  shirika  la Kipalestina  kwa  lengo la  kuonesha  madhila yanayowapata Wapalestina.

Kampeni ya kuisusia Israel

Benjamin Netanjahu, Ministerpräsident Israels | 2017 in Paris
Waziri mkuu wa Israel Benjamin NetanyahuPicha: picture-alliance/AP Photo/S. Nahe

Isreal  imeelezea  kwamba wabunge hao wanaunga  mkono  kile kinachoelezwa  kuwa  ni vuguvugu  linalojulikana  kama  "ususiaji, kutowekeza, vikwazo'', ama BDS, linalounga  mkono Wapalestina. Israel , na  wanasiasa  wengi  wanaounga  mkono  Israel , wanaamini  BDS  ni chuki dhidi ya  Wayahudi na lina nia  ya kuliharibu  taifa  hilo, kitu ambacho wapinzani wanakana.

Seneta kiongozi wa  kundi  la  wachache bungeni Chuck Schumer wa  New York , ambaye  ni Myahudi aliyechaguliwa katika  ngazi hiyo ya juu nchini  humo  na  mmoja  kati ya  watetezi wakubwa, amesema hatua  hiyo  ya  Israel "italeta madhara tu katika  uhusiano  kati ya Israel  na  Marekani na uungaji  mkono  kwa  Israel barani Amerika, na  akaongeza, kuwanyima fursa wabunge wa Marekani  ni ishara  ya  udhaifu, na sio nguvu.