1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Saudi Arabia: Waliomuua Khashoggi kukabiliwa na sheria

Zainab Aziz
25 Oktoba 2018

Kwa mara ya kwanza tangu kuuliwa kwa Jamal Khashoggi, mrithi wa mfalme wa Saudi Arabia Mohammed bin Salman ameahidi kuchukua hatua kisheria ili waliohusika wafikishwe mbele ya mahakama.

https://p.dw.com/p/37Am9
Saudi-Arabien - Saudischer Kronprinz Mohammed bin Salman
Picha: picture alliance/abaca/Balkis Press

Gazeti maarufu  la Wshington Post limeripoti kwamba mkurugenzi  wa shirika la ujajusi la Marekani CIA Gina Haspel alipata wasaa wa kusikiliza kanda ya video juu ya kuuliwa kwa mwandishi habari Jamal  Khashoggi. Hata hivyo gazeti hilo limenukulu vyanzo ambavyo havikutajwa. Mkurugenzi huyo wa CIA alikuwa ziarani  nchini Uturuki aliposikilua kanda hiyo.

Kwa mujibu wa chanzo kimoja ushahidi uliomo kwenye kanda hiyo ni thabiti kabisa na kueleza kwamba  ushahidi huo utazidi kuishinikiza Marekani iiwajibishe Saudi Arabia juu ya kifo cha Khashoggi. Hata hivyo mpaka sasa haijulikani  ni nani aliyempa mkurugenzi wa CIA kanda hiyo. Mpaka sasa Uturuki bado haijathibitisha wala kukanusha ripoti ya gazeti la Washingto Post.

Murugenzi wa shirika la ujasusi la Marekani (CIA) Gina Haspel
Murugenzi wa shirika la ujasusi la Marekani (CIA) Gina HaspelPicha: picture-alliance/Consolidated News Photos/A. Edelmann

Mwanamfalme Mohammed bin Salman mwenye mamlaka yote nchini Saudi Arabia ameahidi kwa uthabiti kwamba waliomuua Khashoggi watafikishwa mbele ya sheria. Hiyo ilikuwa kauli ya kwanza ya mrithi huyo wa mfalme tangu kifo cha mwandishi habari Jamal Khashoggi.

Akihutubia katika hali ya kujiamini mwanamfalme aliwaambia wajumbe waliohudhuria mkutano wa mjini Riyadh wa wewekezaji kutoka duniani kote kwamba lawama nzito zilizotolewa juu ya kuuliwa kwa mwandishi  Khashoggi kwenye ubalozi wa Saudi Arabia mjini Istanbul hazitateteresha juhudi za Saudi Arabia za kuleta mageuzi. Bin Salman alitoa kauli hiyo muda mfupi baada ya rais Donald Trump kunukuliwa na jarida la Wall Street akisema mrithi wa mfalme ambaye kiukweli ni mtawala wa nchi, ndiye anayebeba lawama juu ya operesheni ya kuuliwa kwa Jamal Khashoggi.

Waandamanaji wadai haki kwa mwandishi aliyeuliwa Jamal Khashoggi
Waandamanaji wadai haki kwa mwandishi aliyeuliwa Jamal KhashoggiPicha: picture-alliance/newscom/K. Dietsch

Licha ya mkasa wa Khashoggi eneo kabambe la biashara linaloitwa NEOM limesonga mbele na shughuli za kibishara na  washirika wake. Mkurugenzi mkuu wa mradi huo wa dola bilioni 500 Nadhir al Nasr amesema hayo leo.

Mradi huo uliotangazwa na mwanamfalme mwaka uliopita unaendelezwa katika eneo la kaskazini magharibi mwa Saudi Arabia. Waziri wa nishati Khalid al Falih amesema Marekani itaendelea kuwa mshirika muhimu katika uchumi wa Saudi Arabia licha ya kadhia ya Khashoggi. Hata hivyo idadi kubwa ya wanasiasa na wafanyabaishara wa nchi za magharibi wameususia mkutano juu ya uwekezaji kutokana na kuuliwa Jamal Khashoggi.

Mwandishi:Zainab Aziz/DPA/RTRE

Mhariri: Iddi Ssessanga