1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroQatar

Qatar yaihimiza Israel kusitisha mapigano ukanda wa Gaza

7 Oktoba 2025

Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Qatar amesema kwamba Israel ilipaswa kuwa imesitisha operesheni zake za kijeshi katika Ukanda wa Gaza, kulingana na mpango wa amani uliopendekezwa na Rais wa Marekani Donald Trump.

https://p.dw.com/p/51cGc
Qatar | Doha 2025 | Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Qatar Majed Al-Ansari
Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Qatar Majed Al-AnsariPicha: Imad Creidi/REUTERS

Kauli ya Majed Al-Ansari ameitoa wakati wajumbe wa Hamas na Israel wanaendelea na mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja nchini Misri, wakijadili kuhusu vipengele 20 vya Trump vinavyolenga kuumaliza mzozo wa Gaza.

"Kama taifa linaloshiriki katika zaidi ya juhudi kumi za upatanishi kwa sasa, tunaelewa kuwa mpango wowote wa kufikia makubaliano katika mojawapo ya migogoro hauwezi kuakisi kikamilifu matakwa ya pande zote. Kwa hivyo, ni jambo la kawaida kutarajia kuwepo kwa vipengele ambavyo baadhi ya pande hazitakubaliana navyo."

Baada ya Hamas kukubali Ijumaa iliyopita kujadili suala la kuachiwa kwa mateka chini ya mpango huo, Rais wa Marekani Donald Trump aliihimiza Israeli kusitisha mapigano Gaza, akiandika kwenye mtandao wake wa kijamii wa Truth Social kwamba usitishaji huo wa vita ni muhimu ili kuwaokoa mateka.

Msemaji huyo wa wizara ya mambo ya nje ya Qatar ameeleza matumaini kwamba pande zote mbili - Hamas na Israel – zimejitolea kufikia makubaliano ingawa bado kuna masuala kadhaa yanayohitaji kujadiliwa zaidi.