1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mzozo wa Syria magazetini

9 Septemba 2013

Mzozo wa Syria na Ujerumani kubadilisha msimamo wake dakika ya mwisho,kampeni ya uchaguzi mkuu wa Ujerumani ni miongoni mwa mada zilizochambuliwa zaidi na wahariri wa magazeti ya Ujerumani.

https://p.dw.com/p/19e7I
Kansela Angela Merkel na rais Barack Obama wakihudhuria mkutano wa G-20 mjini St.PetersburgPicha: Reuters/Anton Denisov/RIA Novosti

Tuanzie lakini Syria ambako juhudi za kidiplomasia zimeshika kasi kuanzia wale wanaotaka serikali ya Bashar al Assad "iadhibiwe" kutokana na tuhuma za kutumia gesi ya sumu dhidi ya wananchi wake mpaka kufikia wale wanaoonya dhidi ya hatua kama hizo.

Gazeti la Nordbayerische Kurier la mjini Bayreuth linaandika:

Dunia inatishia kutumbukia katika janga kubwa kabisa la vita.Rais Barack Obama anapiga baragumu la siku tatu za hujuma za kijeshi ili kumrudi muimla wa Syria Bashar al Assad asitumie tena gesi ya sumu iliyowauwa mpaka watoto wadogo.Kansela Angela Merkel ameingiwa na wasi wasi mzozo wa Syria usije ukamvurugia kampeni yake ya uchaguzi.Amejaribu bila ya kufanikiwa kukwepa kuweka saini yake kuunga mkono msimamo wa rais wa Marekani Barack Obama.Kigeu geu hakiashirii mema.Bunge la Marekani-Congress linaweza kuamuacha mkono Obama na matokeo ya dakika ya mwisho yakawa kutofanyika hujuma zozote za kijeshi.

G20 Sankt Petersburg Angela Merkel und Francois Hollande
Kansela Angela Merkel na rais Francois Hollande wa UfaranaPicha: Eric Feferberg/AFP/Getty Images

Mzozo wa Syria na kampeni za uchaguzi Ujerumani

Maoni sawa na hayo yametolewa pia na mhariri wa gazeti la "Nordwest-Zeitung" la mjini Oldenburg anaeandika:

Hivyo sivyo ilivyokuwa imepangwa.Angela Merkel alikuwa ameshaondoka St.Petersburg,bila ya hata kutia saini "waraka kuhusu Syria,kinyume na walivyofanya viongozi wengine wakuu wa Ulaya.Kansela alikuwa nusra ajikute peke yake,kama ilivyowahi kutokea mwaka 2011 kura kuhusu Libya ilipopigwa.Safari hii,kwa bahati nzuri watu wameponea chupu chupu.Kwa kutia saini baadae waraka wakati wa mkutano wa mawaziri wa mambo ya nchi za nje wa umoja wa ulaya mjini Vilnius,mashaka mengi yameweza kuepukwa.Hata hivyo kansela Angela Merkel anabidi ajiulize ilikwenda kwendaje mpaka marafiki zake wa Ulaya wakamwacha peke yake. Alichokifanya hakiwezi kusifiwa kama werevu wa kisiasa.

Deutschland Bundestagwahl 2013 Peer Steinbrück im Bundestag
Mgombea kiti cha kansela wa kutoka chama cha SPD Peer SteinbrückPicha: picture-alliance/dpa

Peer Steinbrück ashinikizwa

Kuna wanaoutaja uamuzi wa kansela katika kadhia hiyo ya Syria kua ni mbinu ya kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu.Kampeni za uchaguzi zimeshika kasi na mgombea kiti cha kansela kutoka chama cha upinzani cha SPD Peer Steinbrück anazongwa na tuhuma za kumuajiri mfanyakazi wa nyumbani miaka 14 iliyopita,bila ya kumlipia kodi ya malipo ya uzeeni wala kodi ya mapato.Ametumiwa barua ya kitisho na kutakiwa ajitoe katika kinyang'anyiro cha kuania kiti cha kansela.Mhariri wa gazeti la "Reutlinger General-Anzeiger" anahisi:

Ni shida kuashiria madhara ya kisa hiki kipya.Kinaweza lakini kuwageukia wale wale walio nyuma ya barua hiyo badala ya kumdhuru Peer Steinbrück.Kwa vyovyote vile mwenyewe Steinbrück ameamua kutokitumia kisa hicho kwa masilahi ya kisiasa au kuwanyoshea kidole wapinzani wake.Hilo pekee linatia moyo.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Inlandspresse

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman