1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yaionya Venezuela kuhusu Guaido

Lilian Mtono
7 Februari 2020

Marekani imeionya serikali ya Venezuela kuhusu kile kinachoweza kuwakabili iwapo kiongozi wa upinzani  Juan Guaido hataruhusiwa kurejea salama nchini humo akitokea ziarani Washington,.

https://p.dw.com/p/3XP0M
Donald Trump empfängt Juan Guaido aus Venezuela
Picha: picture-alliance/abaca/Y. Gripas

Katika kile kilichoonekana kama hatua ya kisasi, serikali ya Caracas iliwazuia kizuizini maafisa sita waandamizi wa shirika la mafuta linaloendeshwa na raia wenye uraia wa Marekani na Venezuela miezi miwili baada ya kuwaruhusu kuhamia kwenye kifungo cha nyumbani.

Mjumbe wa Marekani Elliot Abrams aliyeongoza mpango wa kumuondoa madarakani rais wa Venezuela Nicolas Maduro alionya kwamba Marekani ilikuwa inajiandaa kwa hatua ambazo bado haziko wazi iwapo Guaido atasumbuliwa wakati akirejea nchini humo. Amesema wana wasiwasi mkubwa lakini wana imani atarejea salama.

Guaido anayetambuliwa na Marekani na mataifa mengine mengi ya magharibi pamoja na Marekani ya Kusini kama rais wa mpito wa Venezuela ameapa kuendeleza kampeni zake. "Na ninatangaza, kama nilivyosema asubuhi ya leo kwamba hivi karibuni tutarejea Venezuela kushirikiana na wenzetu kutafuta suluhu ya mzozo, janga na tatizo la kidemokrasia nchini Venezuela. Ninashukuru sana." alisema Guaido.

Hata hivyo amekiri kuwa kuna hatari kubwa kwa kufanya hivyo.

USA Miami Auftritt Guaido Venezuela Parlamentssprecher
Hata hivyo Juan Guaido anahisi hatari kubwa ikimkabili kutokana na hatua zakePicha: Reuters/E. Uzcategui

Guaido wiki iliyopita alikutana na raia wa Venezuela wanaoishi Miami nchini Marekani na baadae kama mgeni wa kushtukiza kwenye hotuba ya rais Donald Trump kuhusu hali ya taifa. Baadae alikutana na Trump kwenye ikulu ya White House.

Serikali ya Maduro inawakosoa vikali Trump na Guaido, lakini huko nyuma ilimruhusu kiongozi huyo wa upinzani kutembea kwa uhuru licha ya juhudi zake za kutaka kuipindua serikali ya Maduro.

Hata hivyo masaa kadhaa baada ya Guaido kukutana na Trump, nchini Venezuela serikali iliwakamata maafisa waandamizi sita wenye uraia pacha, wa Marekani na Venezuela wanaoendesha shirika la mafuta la Marekani la Citgo linalomilikiwa kwa kiasi kikubwa na kampuni ya mafuta ya serikali ya Venezuela ya PDVSA.

Maafisa hao, ambao miezi miwili iliyopita waliruhusiwa kurejea nyumbani, walizuiliwa kwenye mahabusu za idara za usalama za Venezuela, hii ikiwa ni kulingana na familia zao. Mkurugenzi wa shirika lisilo la serikali la Foro Penal linalojihusisha na utetezi wa haki za wafungwa Gonzalo Himiob amesema, walikamatwa ili kujibu tuhuma mpya dhidi yao. 

Kwa mara kwanza walikamatwa mwaka 2017 wakituhumiwa kwa utakatishaji fedha  na makosa mengine ya uhalifu.

Waziri wa mambo ya kigeni wa Urusi Sergei Lavrov aliyeko ziarani Mexico, amekosoa vikali sera za nje za Marekani kuelekea Venezuela pamoja na kile alichoita uchokozi wa Marekani na majaribio ya kuanzisha kisingizio cha uingiliaji wa kijeshi.