Wahariri wazungumzia ziara ya Kansela Merkel nchini Israel
19 Machi 2008
Wahariri wa magazeti ya Ujerumani wamesema katika maoni yao kuwa ziara ya Kansela Angela Merkel pamoja na hotuba yake zimeimarisha hali ya kuaminiana baina ya Israel na Ujerumani.
Hatahivyo baadhi ya wahariri wamesema katika hotuba yake Kansela Merkel angeliweza pia kuzungumzia masuala ambayo si ya kupendeza sana kwa Israel.
Juu ya ziara hiyo mhariri wa gazeti la RHEIN-NECKER anaesifu uhusiano baina ya Ujerumani na Israel ameeleza kuwa kwa kuzingatia historia ya nchi mbili hizo uhusiano huo wa ndani na wa kirafiki ni kama muujiza.
Ziara ya kihistoria ya Kansela Merkel nchini Israel imeimarisha hali ya kuaminiana baina ya waisraeli na wajerumani.
Mhariri huyo ametilia maanani kuwa Kansela Merkel amefuata nyayo za Kansela wa kwanza wa Ujerumani baada ya vita kuu kumalizika, Konrad Adenauer, ambae pamoja na mwanzilishi wa taifa la Israel Ben Gurion waliweka msingi wa mwanzo mpya katika uhusiano baina ya nchi zao.
Gazeti la BERLINER ZEITUNG linasema ziara ya Kansela Merkel iliyofanyika miaka zaidi ya 60 baada ya maangamizi ya wayahudi barani Ulaya, haiwezi kuzingitiwa hasa , kama hatua ya kuufanya uhusiano baina ya Israel na Ujerumani uwe wa kawaida.Mhariri wa gazeti hilo anatathmini ziara hiyo kuwa ni ukurasa mpya katika historia ya watu wa nchi mbili hizo.
Lakini mhariri wa gazeti la LANDESZEITUNG anasema uhusiano baina ya Israel na Ujerumani ungekuwa wa dhati na maalum iwapo pia ungelipewa mtihani kwa kuzungumzia hata masuala ambayo si ya kufurahisha.
Mhariri wa gazeti hilo anatilia maanani katika maoni yake kuwa Kansela Merkel ametumia kauli ya uwazi kabisa kuwalaani Hamas na Iran kwa siasa zao kali dhidi ya Israel.
Lakini gazeti linasema Kansela Merkel pia angeliweza kutumia kauli ya uwazi kuitaka Israel iache kabisa kujenga makao mapya ya walowezi wa kiyahudi katika maeneo ya wapalestina.
Gazeti la NEUES DEUTSCHLAND linalalamika kwamba kansela Merkel ,wala hakuwa na wasaa wa kuyatembelea maeneo ya wapalestina achilia mbali ukweli kwamba katika hotuba yake kiongozi huyo wa Ujerumani, hakutamka neno hata moja juu ya wajibu wa Israel katika mgogoro wa mashariki ya kati.