1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUkraine

Kumbukumbu ya mauaji ya Bucha, miaka minne baadaye

31 Machi 2026

Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Ulaya wahudhuria kumbukumbu ya mauaji ya Bucha na wamekariri nia yao ya kutetea uhuru wa Ukraine

https://p.dw.com/p/5BRwj
Ukraine Bucha 2026 | Kumbukumbu ya miaka 4 ya mauaji ya Bucha
Wadephul asema ujumbe kwa Urusi lazima uwe kwamba wale waliohusika na vita na ukatili wake hawapaswi kuachwa bila kuadhibiwaPicha: Ansgar Haase/dpa/picture alliance

Mawaziri kadhaa wa Mambo ya Nje wa Umoja wa Ulaya wakiongozwa na mwanadiplomasia Mkuu wa umoja huo Kaja Kallas, wamehudhuria kumbukumbu ya miaka minne tangu mauaji ya watu wengi katika mji wa Bucha Ukraine. Mauaji hayo yanadaiwa kufanywa na Urusi ilipoivamia Ukraine.

Kwenye taarifa ya pamoja kwenye kumbukumbu ya miaka minne tangu mauaji ya Bucha yalipofanyika, mawaziri wa mambo ya nje wa Ulaya wamekariri nia yao ya kutetea uhuru wa Ukraine

Mawaziri hao wameeleza kile walichokiita kuwa "dhamira yao isiyoyumba ya kuhakikisha uwajibikaji kamili wa Shirikisho la Urusi, kwa ukiukaji wowote wa sheria za kimataifa nchini au dhidi ya Ukraine".

Msukumo wa Urusi kuwajibishwa kisheria kwa maafa ya Bucha

Akiwa njiani kuelekea Kyiv, mkuu wa sera za kigeni wa Umoja wa Ulaya Kaja Kallas alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha wale waliotoa amri za kuua katika maeneo kama Bucha wanawajibishwa, sawa na wale waliofanya ukatili huo. Umoja wa Ulaya unataka maafa hayo yachunguzwe ili wahusika wawajibishwe kisheria. Vinginevyo, Kallas amesema kunaweza kuwa na kulipizana kisasi.

Mahojiano ya DW | Ukraine | Kaja Kallas kuhusu Bucha na kumbukumbu ya mauaji ya halaiki
Kaja Kallas ashinikiza uwajibikaji dhidi ya waliohusika na mauaji ya halaiki huko Bucha UkrainePicha: Teri Schultz/DW

"Pia ni muhimu kuweka suala la uwajibikaji mezani. Kwa sababu bila uwajibikaji, ikiwa makosa hayo hayatadhibiwa, basi hakuna uwezekano wa kuwa na haki na amani ya kudumu, kwa sababu haki ni sehemu ya mchakato wa amani,” amesema Kallas.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Johann Wadephul aliyekuwa miongoni mwa waliohudhuria kumbukumbu hiyo amesema, mauaji ya Bucha yanasalia kama kidonda kisichopona kwa Waukraine na Ulaya nzima.

Akizungumza katika mji mkuu wa Ukraine, Wadephul alisema Bucha inawakilisha "makosa yaliyokusudiwa dhidi ya raia, na ni sehemu muhimu ya vita vya Urusi dhidi ya Ukraine.

Mzozo wa Ukraine umesahaulika kwa sababu ya mzozo wa Iran?

Huku juhudi zinazoongozwa na Marekani za kumaliza vita zikiwa zimesimama na Washington ikiupa mzozo wa Mashariki ya Kati kipaumbele, serikali za Ulaya zinataka kuendelea kuangazia vita hivyo vya Ukraine ambavyo kwa miongo mingi, ndivyo vikubwa zaidi barani humo na sasa viko katika mwaka wa tano.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ukraine Andrii Sybiha amesema uwepo wa wawakilishi wa Umoja wa Ulaya ni ishara kwamba Urusi haitakwepa kuwajibishwa na haki kwa wahanga itatimia. 

Ukraine, Bucha 2026 | Meya Anatolii Fedoruk awakumbuka wahanga
Kumbukumbu ya Bucha pia ni njia ya kuonesha mshikamano na raia wa Ukraine, mnamo wakati kuna mvutano ndani ya Umoja wa Ulaya kuhusu msaada.Picha: Gleb Garanich/REUTERS

Kulingana na maafisa wa Ukraine na pia mashirika ya kutetea haki za binadamu, vikosi vya Urusi viliwaua zaidi ya watu 400 katika mji mdogo wa Bucha nchini Ukraine.

Ukraine yashambulia vituo vya mafuta vya Urusi

Wakati hayo yakijiri, droni za masafa marefu za Ukraine zilisambaratisha vituo vya mafuta vya Urusi katika Bahari ya Baltiki usiku wa Jumatatu kwa mara ya tano katika kipindi cha zaidi ya wiki moja.

Mashambulizi hayo ni juhudi za Kyiv kujaribu kuzuia Moscow isipate faida kutokana na mauzo yake ya mafuta katikati ya mgogoro wa nishati uliosababishwa na vita vya Iran.

Marekani ililegeza vikwazo vyake dhidi ya mafuta vya Urusina kuruhusu iuzwe mnamo wakati uhaba wa mafuta umechochewa na mkwamo katika mlango wa bahari wa Hormuz.

(DPAE, EBU,RTRE)