Rais wa Ujerumani ataka mageuzi yasonge mbele.
17 Juni 2008
Rais Horst Köhler wa Ujerumani ametoa mwito juu ya kusonga mbele na mageuzi yaliyoleta ustawi wa uchumi na nafasi za ajira nchini Ujerumaji.
Rais Köhler amesema hayo katika hotuba aliyotoa mjini Berlin leo.
Rais Köhler pia amewataka wajerumani wabuni ajenda ya mwaka 2020 ili kufuatilia ajenda ya mageuzi iliyopitishwa chini ya uongozi wa Kansela wa hapo awali Gerhard Schröder iliyokabiliwa na upinzani mkali.
Rais Köhler amesema ajenda ya mageuzi imeleta mafanikio katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita. Kutokana na mageuzi hayo watu zaidi ya milioni moja na laki sita wamerejea kazini ikiwapamoja na wale ambao kwa muda mrefu hawakuweza kupata ajira kwa muda mrefu kutokana na umri wao mkubwa.
Juu ya elimu kiongozi huyo wa Ujerumani amesema Ujerumani inahitaji kujenga mazingira ambapo elimu itatambulika. Amewataka wajerumani wajenge nchi inayoheshimu elimu- nchi ambapo wanaofanya juhudi za kutafuta elimu wanaheshimiwa. Amesisitiza umuhimu wa kuleta utengemano wa kijamii baina ya wananchi wote . Ameeleza kuwa utengemano huo pia unapaswa kuhimizwa baina ya vijana na wazee na baina ya watu wa mijini na wa mashambani.
Rais wa Ujerumani pia amesema pana haja ya kuleta mageuzi katika taasisi za kisiasa ili ziweze kueleweka na wananchi na hivyo kuweza kuepusha kutamauka kisiasa kwa wananchi wengi na kutokana na hayo ametaka kufanyika kwa mageuzi katika mfumo wa kodi na wa uchaguzi. Katika hotuba yake ya kila mwaka kiongozi huyo wa Ujerumani amelaumu jinsi demokrasia inavyotekelezwa nchini Ujerumani na ameshauri kufanyika mabadiliko katika mfumo wa uchaguzi.