1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Biden kuipa Kenya hadhi ya mshirika mkuu nje ya NATO

24 Mei 2024

Rais Joe Biden wa Marekani amesema ataifanya Kenya kuwa mshirika mkuu asiye mwanachama wa Jumuiya ya NATO, hadhi ambayo imetolewa kwa mataifa kama vile Qatar na Israel.

https://p.dw.com/p/4gEH0
Marekani | Joe Biden amkaribisha William Ruto
Rais Joe Biden wa Marekani (kulia) akiwa na mgeni wake, Rais William Ruto wa Kenya.Picha: Susan Walsh/AP Photo/picture alliance

Biden aliyasema hayo siku ya Alhamisi (Mei 23) alipomkaribisha Rais William Ruto wa Kenya katika ikulu ya White House, akiwa kwenye ziara rasmi inayolenga kukabili ushawishi wa Urusi na China barani Afrika. 

Biden alisema hatua hiyo inatimiza ahadi ya miaka kadhaa ya ushirikiano dhidi ya makundi ya Al-Shabaab na lile linalojiita Dola la Kiislamu nchini Somalia. 

Soma zaidi: Biden, Ruto waahidi kulinda demokrasia Afrika na kwingineko

"Operesheni zetu za pamoja za kukabiliana na ugaidi zimedhoofisha nguvu za ISIS na al-Shabaab kote Afrika Mashariki. Msaada wetu wa pande zote kwa Ukraine umehamasisha ulimwengu kusimamia Mkataba wa Umoja wa Mataifa. Na kazi yetu ya pamoja nchini Haiti inasaidia kuweka njia ya kupunguza hali ya ukosefu wa utulivu na usalama." Alisema Biden,

Sikiliza: 

Ziara ya Ruto Marekani ina maslahi gani?

Hatua hiyo itaifanya Kenya kuungana na mataifa mengine 18 yenye hadhi kama hiyo, yakiwemo Israel, Brazil na Ukraine, na hivyo kuimarisha ushirikiano wa kijeshi na kidiplomasia, ingawa hakutakuwa na makubaliano rasmi ya kiusalama. 

Biden pia aliishukuru Kenya kwa kukubali kuongoza kikosi cha polisi wa kimataifa nchini Haiti, ambako magenge ya uhalifu yameliingiza taifa hilo la Karibia katika mzozo wa kisiasa na kiutu.