1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wapalestina 40 wauawa Gaza kwa mashambulizi ya Israel

12 Septemba 2025

Mamlaka za afya za Ukanda wa Gaza zimesema watu wasiopungua 40 wameuawa Ijumaa kutokana na mashambulizi ya Israel. Mamlaka za afya zaUkanda huo zimesema vifo vingi vimeripotiwa katika jiji la Gaza.

https://p.dw.com/p/50PoU
Ukanda wa Gaza
Muonekano wa sehemu ya jiji la Gaza baada ya mashambulizi ya IsraelPicha: Jack Guez/AFP/Getty Images

Shambulio moja la anga katika jiji la Gaza pekee limewauwa watu 14 waliokuwa ndani ya nyumba moja. Jeshi la Israel limesema litachunguza kuhusu ripoti   mauaji hayo.

Licha ya ahadi hiyo msemaji wa jeshi hilo amechapisha orodha ya maeneo yote ambayo wakaazi wa Gaza wanaweza kukimbilia wakati Israel ikijiandaa kuudhibiti mji huo.

Mmoja wa wakaazi wa Gaza Wahid Al Ras kama ilivyo kwa wakaazi wengi wa eneo hilo amelaani amri hiyo ya Israel akisema, "Hata kama tunataka kuondoka, tunakwenda wapi? Hakuna nafasi. Wanakwambia nenda kusini lakini wala hakuna nafasi. Huko wanakodisha mita moja ya mraba kwa dola 3.61. Hatuna pesa. Kama mtu anataka tuhame na atuhamishe atupe mahali salama pa kwenda. Nchi 22 za Kiarabu hazituulizii, hakuna anayeuliza kuhusu sisi. Tumekuwa vitani kwa miaka miwili na hakuna anayetuangalia"

Israel imesema inachukua hatua hiyo dhidi ya wanamgambo wa Hamas na makundi mengine ya magaidi kwenye mji huo ili kuepuka idadi kubwa ya vifo vya raia. Mashirika ya misaada hata hivyo yanaonya kuwa hatua hii itazidisha hali mbaya ya kiutu inayowakabili raia.

UAE yatoa karipio rasmi kwa Israel

Hayo yakiendelea Umoja wa Falme za Kiarabu umesema ulimwita naibu balozi wa Israel nchini humo mapema leo na kumpa karipio rasmi kuhusu shambulio lililofanywa na jeshi la nchi yake mjini Doha. Wizara ya mambo ya nje imesema Waziri wa Ushirikiano wa Kimataifa wa Falme za Kiarabu Reem bint Ebrahim Al Hashimy, ameutumia mkutano wake balozi David Ohad Horsandi kulilaani shambulio hilo pamoja na kauli za Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu.

Doha, Qatar 2025
Jengo lililoharibiwa baada ya mashambulizi ya Israel dhidi ya viongozi wa Hamas mjini DohaPicha: Ibraheem Abu Mustafa/REUTERS

Kwingineko Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio anatarajiwa kuelelekea Israel Jumamosi wakati huu kukiwa na mivutano Mashariki ya Kati baada ya shambulio la la Israel mjini Doha lililowalenga viongozi wa Hamas. Ziara hiyo imepangwa wakati Baraza Kuu la Umoja Umoja wa Mataifa likiwa limepitisha azimio linalounga mkono kuundwa kwa taifa huru la Palestina lakini bila ya uwepo wa kundi la Hamas.