1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vita vya Maneno kati ya Donald Trump na Kim Jong-un

Oumilkheir Hamidou
15 Agosti 2017

Vita vya maneno kati ya Rais Donald Trump wa Marekani na kiongozi wa Korea ya Kaskazini Kim Jong-un, na sura ya muungano baada ya uchaguzi mkuu wa september 24 nchini Ujerumani ni miongoni mwa mada magazetini.

https://p.dw.com/p/2iE6G
Donald Trump und Xi Jinping
Picha: picture alliance/AP Photo/S. Loeb/Pool Photo

Tunaanza na kitisho cha vita vya maneno kati ya rais wa Marekani Donald Trump na mtawala wa Korea ya Kaskazini Kim Jong-un. Gazeti la "Emder" linamulika enzi za rais wa Marekani Donald Trump na kuandika: "Miezi saba imeshapita tangu aingie madarakani. Tangu miezi saba sasa anautia kishindo ulimwengu na kuwaweka katika hali ya wasi wasi mamilioni ya watu nchini mwake. Donald Trump anafuata njia ya hatari inayokwenda kinyume na itifaki ya kidiplomasia. Ni sawa kwamba mtawala wa Korea ya Kaskazini, Kim Jong-un anapalilia moto. Lakini maneno makali yanayotolewa na rais wa Marekani kupitia risala zake katika mtandao wa Tweets yanachochea hatari ya kuripuka vita.

Si hayo tu, lakini tajiri huyo mkubwa mwenye mdomo mpana anazidisha balaa kwa kuiwekea Venezuela pia bastola kifuani. Lakini  anakosa la maana la kusema vinapohusika vitimbi vya wafuasi wa siasa kali za mrengo wa kulia, kama vile vilivyoshuhudiwa hivi karibuni Charlottesville. Hali hiyo inamaanisha kushindwa kwake kisiasa, tangu nje mpaka ndani ya nchi hiyo."

China yaitia kishindo Korea ya kaskazini

Mzozo uliozushwa na Korea ya Kaskazini unaisumbua pia nchi jirani na mshirika-China. Gazeti la "Landeszeitung" linaandika: "Mtu anaweza kufikiria kwamba si kiongozi wa ikulu ya Marekani aliyekishinikiza chama cha kikoministi cha China kutishia kukilisha hasara ya thuluthi moja ya mapato yanayotokana na biashara yake ya nje chama ndugu cha mjinim Pyongyang. Uamuzi huo unadhihirisha kwamba Peking, inaendelea kufuata mkakati ule ule wa kujionyesha mbele ya ulimwengu na majirani zake kama nchi ya nia njema na ambayo iko tayari kubeba majukumu zaidi.

Lakini kuambatana na maazimio ya umoja wa Mataifa, China inacheza na moto. Hakuna kinachohofiwa na Peking kuliko kuibuka nchi inayosumbuliwa na njaa, itakayopelekea wimbi la wakimbizi kuelekea katika maeneo yake ya mpakani. Kile ambacho watu hawakitarajii ni kuziona China na Korea ya Kusini zikijiachia kuwa wasaidizi wa kudumu wa Korea ya Kaskazini."

Muungano wa aina gani baada ya september 24 Ujerumani?

Kampeni za uchaguzi mkuu zimepamba moto nchini Ujerumani. Kilichohanikiza zaidi ni nani atashirikiana na nani kuunda serikali ya muungano baada ya uchaguzi mkuu september 24 inayokuja. Gazeti la "Badische Neueste Nachrichten" linaandika: "Kwa kuwa muungano wa kawaida wa pande mbili itakuwa shida kuundwa pamoja na FDP au na walinzi wa mazingira ni Grüne, njia iliyoibuka badala ya muungano wa vyama vikuu ambao hakuna anaetaka kuusikia ukitajwa, ni ile ya muungano wa vyama vitatu au Jamaica kama unavyoitwa kwa kuzingatiwa rangi ya bendeza ya nchin hiyo.

Hata kwa kuzingatia masilahi ya kijamii  na kiuchumi muungano kama huo wa vyama vitatu unavutia na unaweza kuangaliwa kama njia mpya inayomfungulia Angela Merkel fursa ya kuingia katika mhula wake wa nne madarakani na wakati huo huo kuvihakikishia vyama ndugu vya CDU/CSU wingi wa viti bungeni. SPD ndio wanaojiuliza hali itakuwa ya aina gani baada ya uchaguzi mkuu."

 

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Inlandspresse

Mhariri: Mohammed Khelef