1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Janga

Urusi yasema itaendelea kujiimarisha Ukraine

17 Desemba 2025

Rais wa Urusi Vladimir Putin ameonya kuwa nchi yake itaendelea kujiimarisha katika ardhi ya Ukraine, iwapo Kiev na washirika wake wa Magharibi watayakataa masharti ya Kremlin katika mazungumzo ya amani ya Ukraine.

https://p.dw.com/p/55Ydz
Russland Moskau 2025 | Vladimir Putin
Rais wa Urusi Vladimir PutinPicha: Russian President Press Office/ZUMA/picture alliance

Akizungumza katika mkutano wake wa kila mwaka na maafisa wakuu wa jeshi, Putin amesema angelipenda kutatua hali kidiplomasia, lakini iwapo matakwa yao yatakataliwa, iko tayari kutumia nguvu kuokoa maeneo yake.

Huku hayo yakiarifiwa Rais wa Halmashauri Kuu ya Umoja wa Ulaya Ursula Von der Leyen, amesema Ulaya inapaswa kuwajibika yenyewe katika masuala yake ya usalama huku akisema ni lazima ichukue hatua kuhakikisha amani inapatikana Ukraine.

"Tutaendelea kufanya kazi kwa karibu na Rais Zelensky na Rais Trump kufikia kile sote tunachokitaka, amani ya kudumu ambayo inalinda uhuru wa Ukraine na kuimarisha usalama wake. Mbinu yetu iko wazi kabisa na tunafanya kazi kwa nguvu zetu zote ili kusitisha umwagaji damu. Hatua ya kwanza ni usitishaji mapigano na njia ya kufika huko inajulikana. Urusi lazima ishinikizwe kuja katika meza ya mazungumzo sio kwa kujionesha tu, bali kwa vitendo na matokeo."

Viongozi wa Ulaya wapo katika shinikizo la kutumia mali ya Urusi iliyozuiliwa kuifadhili Ukraine na kuishinikiza Moscow kuingia katika meza ya mazungumzo na kumaliza vita vyake Kiev.