Trump asema vita dhidi ya Iran vinakaribia kumalizika
2 Aprili 2026
Rais wa Marekani Donald Trump ametetea msimamo wake wa kushambulia Iran katika hotuba yake ya kwanza kwa taifa, ikiwa ni zaidi ya mwezi mmoja tangu vita kuanza, akisisitiza kwamba Marekani iko karibu kushinda huku kiwango chake cha uungwaji mkono kikiporomoka.
Katika hotuba ya jana jioni kutoka Ikulu ya White House, Trump hakutoa maelezo mapya kuhusu jinsi vita hivyo vitakavyomalizika, lakini aliapa kwamba Iran itakabiliwa na mashambulizi makali zaidi kwa muda wa wiki mbili hadi tatu zijazo.
Trump alisema kwamba Marekani inalenga kulisambaratisha jeshi la Iran, kukomesha uungaji mkono wa taifa hilo linalotawaliwa kidini kwa makundi yenye silaha katika kanda hiyo na kuizuia kuunda silaha za nyuklia, jambo ambalo wakaguzi wa nyuklia wa Umoja wa Mataifa na wachambuzi wengi wanasema halikuwa karibu kutokea.
Hotuba ya Trump kwa kiasi kikubwa iliakisi machapisho ya kila siku anayoyoandika katika mitandao yake ya kijamii na mahojiano ya kila mara na vyombo vya habari.