1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Sudan yakaribisha matamshi ya Pompeo

Sekione Kitojo
2 Agosti 2020

Serikali ya Sudan imekaribisha  matamshi yaliyotolewa na waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Mike Pompeo wiki hii kwamba angependa kuiondoa Sudan kutoka katika orodha ya nchi zinazofadhili ugaidi.

https://p.dw.com/p/3gHsD
USA Mike Pompeo
Mike Pompeo , waziri wa mambo ya kigeni wa MarekaniPicha: Getty Images/M. Ngan

Pompeo mara kwa mara  ameashiria  kwamba  wizara ya mambo ya kigeni  inamatumaini  ya kuondoa sifa hiyo, ambayo  inazuwia kwa kiasi  kikubwa  uwekezaji nchini Sudan, lakini mzozo umejitokeza kuhusiana  na  malipo ya  fidia kuhusiana  na  shambulizi la bomu mwaka  1998 katika  balozi  mbili  za  Marekani.

Bundespräsident Steinmeier im Sudan
Waziri mkuu wa Sudan Abdalla HamdokPicha: picture-alliance/dpa/B. von Jutrczenka

Mwanadiplomasia  huyo  wa  ngazi ya juu  wa  Marekani  ameiambia kamati ya  mahusiano  ya  nje  ya  baraza  la  Seneti siku  ya Alhamis kuwa  sheria  kuhusiana  na  malipo  hayo yanapaswa kuwasilishwa  mbele  ya  bunge  la  Marekani Congress,"katika kipindi , cha hivi  karibuni  kabisa".

Kwa mujibu wa  ripoti kwa lugha  ya  Kiingereza ya  shirika  rasmi  la habari  la  Sudan SUNA, serikali ya  mpito  ya  Sudan, imekaribisha jana  Jumamosi  taarifa  ya  Pompeo  na "kuahidi kufanya  kila linalowezekana kutimiza  mahitaji  ambayo  yatasaidia  utawala  wa Marekani "kuchukua " hatua sahihi".

Jukwaa  la  taarifa  huru  katika  inteneti la Sudan  Tribune  limeripoti kuwa  serikali  imesema  katika  taarifa  kuwa iko "tayari kuendelea kufanyakazi na  utawala  wa  marekani  kuiondoa  Sudan  kutoka katika  orodha ya  mataifa  yanayofadhili  ugaidi  na  kuingia  katika uhusiano  wa  ushirikiano  ambao  utazifaidia nchi zote mbili".

Sudan‚ Soldaten
Ulinzi ulioimarishwa katika taasisi ya sayansi ya sheria na mahakama kwa ajili ya kesi ya rais wa zamani wa Sudan Omar Hassan al-Bashir mjini KhartoumPicha: picture-alliance/AA/M. Hjaj

Kuanguka kwa dikteta Sudan

Pompeo  amesema  kuwa  kuanguka  kwa  dikteta wa muda  mrefu Omar al-Bashir kufuatia  maandamano  makubwa  na  serikali inayokaribia  kutimiza  mwaka  mmoja  sasa  inayoongozwa  na waziri  mkuu  raia, Abdalla Hamdok, ni " fursa  ambayo  haiji  mara kwa  mara".

"Kuna nafasi  sio tu kwa demokrasia  kuanza  kujengwa, lakini huenda  fursa za  kimkoa  ambazo zitamiminika  kutokana  na  hilo pia," amesema.

"Nafikiri  kuondoa sifa ya taifa linalofadhili ugaidi nchini humo iwapo tutaweza, kuhudumia wahanga wa maafa  hayo itakuwa  jambo  zuri kwa  sera za  kigeni  za  Marekani," Pompeo alisema.

Kwa mujibu  wa  shirika  la habari la  Sudan SUNA , Hamdok alisisitiza, "nia  yake ya kuendelea  kuweza  juhudi pamoja  na marafiki wote nchini  Marekani  na  kwingine" kufikisha  mwisho suala  hilo  na  kwa  Sudan kurejea  kikamilifu kuwa "sehemu ya jumuiya  ya  kimataifa".

Sudan Umar Hassan Ahmad al-Bashir PK nach dem Putscht
Kiongozi wa mapinduzi Omar Hassan al-Bashir akitangaza kuundwa kwa serikali mpya Julai 8, 1989 mjini KhartoumPicha: Getty Images/AFP/M. Nelson

Bashir alimkaribisha  kiongozi  wa  al-Qaeda Osama bin Laden  na Sudan  ilishutumiwa  kusaidia  wanajihadi  ambao waliripua  balozi nchini  Kenya  na  tanzania, wakiwauwa watu 224  na  wengine 5,000  walijeruhiwa.

Serikali  mpya  ya  Sudan  imekubali kutoa  malipo  ya  fidia  lakini mzozo umezuka kuhusiana  na  malipo  makubwa  kwa Wamarekani kuliko  Waafrika, ambao  idadi  ya wahanga  ilikuwa  kubwa  zaidi.