1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Shirika la IAEA laikosoa Iran kwa kukwamisha kazi zake

Sudi Mnette
8 Septemba 2021

Shirika la kimatafa la kudhibiti silaha za nyuklia IAEA (08.09.2021) limetoa ripoti yenye inayosema serikali ya Iran inakwamisha kazi zake za upekuzi wa shughuli za nyuklia.

https://p.dw.com/p/404B8
Generaldirektor der Internationalen Atomenergiebehörde IAEA, Rafael Mariano Grossi aus Argentinien
Picha: Lisa Leutner/AP Photo/picture alliance

Ripoti hiyo imetolewa wakati juhudi za kidiplomasia za kujaribu kuufufua mkataba wa nyuklia uliosainiwa 2015 kati ya Iran na mataifa yenye nguvu duniani zikiwa bado katika mkwamo. Imesema pia Iran imeongeza urutubishaji wa madini ya urani kupindukia kiwango kilichokubaliwa katika makubaliano ya 2015.

Katika ripoti nyingine ya pili iliyochapishwa pia hapo awali shirika la IAEA limesema hakujapatikana ufanisi mkubwa katika masuala mengine kuhusu uwezekano wa shughuli za nyuklia katika vinu kadhaa nchini Iran ambazo huenda hazijatangazwa.

Iran imesitisha shughuli za Ukaguzi za Shirika la kimatafa la kudhibiti silaha za nyuklia.

Iran Urananreicherungsanlage in Natanz
Kinu cha nyuklia cha Nantaz, IranPicha: AEOI/ZUMA Wire/imago images

Mwezi Februari Iran ilizisitisha baadhi ya shughuli za ukaguzi za shirika IAEA ikitajwa kuwa ni kuijibu Marekani, kwa kukataa kuliondolea taifa hilo vikwazo lakini pia kulidhibiti shirika hilo kuvifikia vifaa vya ukaguzi kama kamera. Awali Iran ilifikia makubaliano ya muda na shirika hilo, ambapo ilikubali kuvitunza vifaa hivyo vya kurekodi kumbukumbu na baadae kuvikabidhi kwa shirika hilo la Umoja wa Mataifa la kuchunguza nguvu za atomiki duniani.

Hata hivyo kwa mujibu ya ripoti hiyo mpya, makubaliano hayo yalipitwa na wakati Juni 24, na Iran ikashindwa kabisa kujihusisha na shirika hilo katika makubaliano katika muda wa miezi kadhaa.

Ripoti inasema tangu Feburuari 23, shughuli za uhakiki na ufuatiliaji wa shirika hilo zimevurugwa sana kutokana na uamuzi wa Iran wa kusimamisha utekelezaji wa ahadi zake zinazohusiana na mpango wake wa nyuklia. Chanzo kimoja cha kidiploamsia kimesema kwa kawaida vifaa hivyo vilikuwa vikifanyiwa ukarabati kila baada ya miezi mitatu lakini kwa sasa kumesalia hoja kama mifumo yote inafanya kazi.

Kamera za uangalizi zimetajwa kuvunjwa na nyingine kuteketezwa kabisa.

Iran Hassan Rouhani und Ali Akbar Salehi
Rais aliyepita wa Iran Hassan Rouhani und mkuu wa zamani wa AEA, Ali Akbar Salehi Picha: Office of the Iranian Presidency/AP Photo/picture alliance

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, moja kati ya kamera zilizopo katika karakana ya mji wa Karaj imeteketezwa na nyingine kuharibiwa vibaya. Televisheni ya taifa ya Iran na shirika lingine la habari nchini humo Tasnim kwa pamoja yaliripoti kwamba Juni kulitokea kile ilichokiita operesheni za hujuma kutokea katika jengo moja lililopo karibu na jengo linalomilikiwa na shirika la nguvu za atomiki mjini Karaj.

Mkurugenzi Mkuu wa IAEA Rafael Grossi aliwahi kutangaza kuwa yupo huru kwa kupata nafasi ya kukutana na  serikali ya Rais mpya wa kihafidhina wa taifa hilo, Ebrahim Raisi, lakini hata hivyo hakujawahi kufanyika ziara ya aina hiyo, na kwamba chanzo kimoja cha kidiplomasia kinasema Iran inaonekana haina utayari wa kufanya mazungumzo yoyote na IAEA.

Iran imeongeza nguvu ya urutubishaji wa kupinduka kiwango kilichoridhiwa 2015.

Ripoti inasema Iran imeongeza nguvu ya hazina yake ya urutubishaji wa kupinduka kiwango ambacho kiliridhiwa mwaka 2015, kwa makubaliano ya kile kilichofahamika kama Mpango  wa pamoja na Utekeletaji (JCPOA).  Kwa zingatio la mpango huo Iran ilipewa fursa ya kupunguziwa vikwazo na mataifa ya Magharibi na Umoja wa Mataifa kwa kuudhibiti mpango wake wa nyuklia.

Baada ya Rais aliyepita wa Marekani kujiondoa katika makubaliano ya nyuklia ya 2015, mrithi wake Joe Biden anataka kulirudisha taifa hilo tena. Lakini Iran kwa sasa inasisitiza vikwazo vyote ilivyowekewa na Marekani tangu 2017 viondolewe. Hali ilivyo sasa kwa mujibu waIAEA inatishia usalama.

Marekani imesema mjumbe wake maalumu kwa Iran, Robert Malley, na ujumbe mdogo watakwenda Moscow na Paris juma hili, kwa ajili ya mashauriano na washirika wao wa Urusi na Ulaya kuhusu mpango ya nyuklia wa Iran na kutapaswa kuwepo na uhitaji wa kufikiwa makubaliano ya haraka na utekelezaji wa kurejea kwa pamoja katika makubaliano ya Mpango wa Pamoja wa Utekelezaji (JCPOA).

Chanzo: AFP