1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUrusi

Putin aahidi kuwa malengo ya kijeshi ya Kremlin yatatimizwa

19 Desemba 2025

Rais wa Urusi amesema kwamba wanajeshi wa nchi hiyo wanaendelea kusonga mbele katika uwanja wa vita, akieleza matumaini kwamba malengo ya kijeshi ya Kremlin yatatimizwa karibu miaka minne baada ya kuivamia Ukraine.

https://p.dw.com/p/55ivx
Urusi | Moscow 2025 | Vladimir Putin
Rais wa Urusi Vladimir PutinPicha: Gavriil Grigorov/REUTERS

Akizungumza katika mkutano wake wa mwisho wa mwaka na vyombo ya habari, Vladimir Putin ametangaza kwamba vikosi vya Urusi vimepiga hatua kubwa ya kimkakati na kwamba vikosi hivyo vitapata mafanikio zaidi kabla ya mwisho wa mwaka.

Putin ambaye ameitawala Urusi kwa miaka 25, ameutumia mkutano huo kuimarisha mamlake yake na kueleza mtazamo wake kuhusu masuala ya ndani ya nchi hiyo na kimataifa.

Amesisitiza kwamba Moscow iko tayari kwa suluhu ya amani itakayoshughulikia sababu za msingi za mzozo kati yake na Ukraine - kauli inayoashiria masharti magumu ya Kremlin kwa makubaliano yoyote ya amani.

"Sio sisi tunaowapiga vita ni nyinyi mnaotupiga vita kupitia askari wa Ukraine. Tuko tayari kusitisha uhasama huu mara moja, huku tukihakikisha usalama wa Urusi kwa muda wa kati na mrefu. Na tuko tayari kushirikiana nanyi."

Mapema wiki hii, Putin alionya kwamba Urusi itaendelea kusonga mbele zaidi ndani ya Ukraine iwapo Kyiv na washirika wake wa Magharibi watakataa madai ya Kremlin.