1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Nicaragua yataka Ujerumani isiiuzie silaha Israel

Lilian Mtono
8 Aprili 2024

Nicaragua imeiomba Mahakama ya Kimataifa ya Haki, ICJ kuiagiza Ujerumani kuacha kuiuzia silaha Israel.

https://p.dw.com/p/4eYML
Niederlande | Internationaler Gerichtshof in Den Haag | Nicaragua gegen Deutschland
Picha: Robin van Lonkhuijsen/ANP/picture alliance

Nicaragua pia imetaka kuangaziwa upya uamuzi wa kusitishwa ufadhili kwenye Shirika la Wakimbizi wa Kipalestina, UNRWA, huku ikisistizia kitisho kikubwa cha mauaji ya kimbari katika Ukanda wa Gaza.

Balozi wa Nicaragua nchini Uholanzi Carlos Jose Arguello Gomez ameiambia mahakama hiyo kamba Ujerumani imekiuka Mktaba wa Mauaji ya Kimbari wa mwaka 1948, kwa kuendelea kuipatia silaha Israel baada ya majaji wa ICJ kutoa uamuzi kwamba inaaminika Israel ilikiuka baadhi ya haki zilizomo kwenye mkataba huo kufuatia mashambulizi yake huko Gaza. 

Carlos Jose Arguello Gomez ni Balozi wa Nicaragua na alisema, "lakini hata katika hali mbaya sana machafuko, serikali inapaswa kuheshimu kanuni za sheria za kimataifa. Mheshimiwa Rais, kwa kuzingatia misingi au ufafanuzi wowote, kinachojulikana kama haki ya kujilinda hakiwezi kamwe kuhalalisha ukiukaji wa kanuni za Mkataba wa Mauaji ya Kimbari au kanuni nyingine za sheria za kimataifa za kibinadamu. Inashangaza, Ujerumani ni kama haiwezi kutofautisha kati ya kujilinda na mauaji ya halaiki."

Gomez amesema, chini ya mkataba huo mataifa yaliyotia saini kama Ujerumani yana wajibu wa kuzuia mauaji ya kimbari.