1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Korea Kaskazini yailaumu Marekani kwa kuchochea vita

Zainab Aziz
2 Mei 2017

Korea Kaskazini imeilaumu Marekani kwa kuendelea kuisukuma rasi ya Korea kuingia katika vita vya nyuklia. Lawama hizo ni baada ya Marekani kufanya mazoezi pamoja na vikosi vya anga vya Korea Kusini na Japan. 

https://p.dw.com/p/2cDca
Südkorea US Kampfflugzeuge über Osan Air Base
Picha: picture-alliance/AP Photo/L. Jin-man

Katika mazoezi hayo ndege mbili za kivita zenye kasi kubwa aina ya B-1B Lancer zilitumika huku hali hiyo ikiongezea mvutano kuongezeka juu ya Korea ya Kaskazini na harakati zake za kufanikisha mipango yake ya makombora ya nyuklia pia katika muendelezo wake wa kukiuka vikwazo ilivyowekewa na Umoja wa Mataifa vilevile kutokana na shinikizo la Marekani dhidi ya nchi hiyo.

Rais wa Marekani Donald Trump amesema kuwa yuko tayari kukutana na rais wa Korea Kaskazini Kim Jong Un huku mkuu wa shirika la ujasusi la Marekani CIA akiwa amewasili nchini Korea Kusini kwa ajili ya mazungumzo. Trump lakini hakusema ni masharti gani Korea Kaskazini inahitaji kuyatimiza kabla ya kukutana na kiongozi wa Korea Kaskazini.

USA Donald Trump
Rais wa Marekani Donald TrumpPicha: Getty Images/O. Douliery

Rais wa Marekani Donald Trump alionya siku ya Jumatatu kwamba upo uwezekano mkubwa wa kutokea vita na Korea Kaskazini huku China ikisema kuwa hali kama hiyo katika rasi ya Korea inaweza kufikia kiwango ambacho si rahisi kudhibiti kutokea machafuko.

Msemaji wa wizara ya ulinzi ya Korea Kusini Moon Sang-gyun aliwaambia waandishi wa habari kwamba zoezi la kijeshi la pamoja lililofanyika siku ya jumatatu lililenga kuzuia uchokozi wa Korea Kaskazini na vilevile lilikuwa ni zoezi la kujiweka tayari kutokana na uwezekano wa majaribio mengine ya nyuklia kutoka Korea kaskazini. Kikosi cha jeshi la anga la Marekani kimesema ndege hizo za kivita ziliruka katika anga ya Guam wakati wa kufanya mazoezi hayo ya kijeshi pamoja na wanaanga wa Korea Kusini na wa Japan.

Korea Kaskazini imesema mazoezi hayo ya kudondosha mabomu ya nyuklia yamefanyika katika anga yake wakati rais Donald Trump pamoja na wenzake wapenda vita wakijiandaa kuishambulia nchi yake kwa silaha za nyuklia na kwamba zoezi hilo la kijeshi ni uchokozi unaochochea hali ya kuzuka kwa vita katika rasi ya Korea.

Kimsingi Korea Kaskazini na Korea Kusini bado zimo katika vita baada mgogoro wa mwaka 1950 hadi mwaka 1953 vita ambavyo vilimalizika baada ya kufikiwa makubaliano ya kusimamisha mapigano baina ya nchi hizo mbili lakini Korea Kaskazini imekuwa ikiendelea kuitishia kuishambulia Marekani, Japan na Korea Kusini.

Mwandishi: Zainab Aziz/RTRE

Mhariri:Iddi Ssessanga