1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Korea Kaskazini imesema imefanya "jaribio muhimu sana"

Sudi Mnette
8 Desemba 2019

Korea Kaskazini imesema (08.12.2019) imefanya jaribio la roketi ya masafa marefu, ikieleza kwamba litakua matokeo muhimu katika eneo lake la kimkakati.

https://p.dw.com/p/3UP4S
Nordkorea Waffentest
Picha: picture-alliance/AP Photo/KCNA

Shirika la Habari la Korea CNA limesema jaribio hilo limefanywa katika eneo la maalumu la kufanyia majaribio la Sohae. Na kuongeza kwamba matokeo ya jaribio husika yameripotiwa kamati kuu ya chama tawala cha taifa hilo. Hata hivyo ripoti haikuisema jaribio lenyewe lilikuwaje hasa.

Lakini vyombo vya habari vimesemea  picha mpya ya satellite inaonesha Korea Kaskazini inaweza kuwa inajiandaa kuanzisha upya mtambo ambao unatumika kusukuma satellite katika eneo hilo. Ripoti za jaribio hilo zinatolewa katika kipindi ambacho Korea Kaskazini imeongeza shinikizo kwa Marekani kuonesha jitihada za wazi katika katika mazungumz yaliokwama ya nyuklia.

Marufuku ya Umoja wa Mataifa kwa Korea Kaskazini

Nordkorea Raketentest
Televisheni ya umma ikionesha picha za komboraPicha: Reuters/H. Ran

Umoja wa Mataifa uliipiga Marufuku Korea Kaskazini kurusha satellite kwa sababu, inalichukulia jambo hilo kama jaribio la jaribio la makombora ya masafa marefu. Baada ya kufanya majaribio kadhaa yalioshindwa, Korea Kaskazini ilifanikiwa kuifikisha satellite yake katika mzunguko wa dunia mwaka 2016.

Katika taarifa yake iliyotolewa kwa Umoja wa Mataifa, balozi wa Korea katika umoja huo, Kim Song alisema mjadala wa kuachana na matumizi ya nyuklia umekwishaondolewa katika meza ya mazungumzo. Taarifa hiyo iliongeza kwa kusema Korea Kaskazini haiitaji mjadala mrefu na Marekani. Hayo yakizingatia kumalizika kwa muda uliopangwa wa mazungumzo hayo wa mwisho wa mwaka kati ya kiongozi wa Korea Kaskazini na wawakilishi wa Marekani.

Taarifa ya Song inatajwa kuwa ni majibu ya lawama kutoka kwa mataifa sita ya Ulaya kuhusu kufanya majaribio 13 ya makombora tangu Mei. Mataifa hayo ni Ufaransa, Ujerumani, Uingereza, Ubelgiji, Poland na Estonia. Korea Kaskazini imesema hatua ya mataifa hayo kuilaani ni uchokozi mwingine dhidi ya Korea.