Khamenei amshutumu Trump kwa vifo vilivyotokea Iran
17 Januari 2026
Kiongozi mkuu wa Iran, Ayatollah Ali Khamenei, amesema mamlaka nchini humo ni lazima zizime nguvu za watu wanaochochea ghasia huku akimshutumu Rais wa Marekani Donald Trump kwa vifo vilivyotokea baada ya ukandamizaji wa wimbi la maandamano dhidi ya utawala wa nchi hiyo.
Khamenei ameongeza kwa kusema kwamba hawana nia ya kuitumbukiza nchi vitani, lakini hawatoacha kuwashughulikia wahalifu wa ndani. Alikuwa akizungumza na wafuasi wake wakati wa hotuba ya kuadhimisha sikukuu ya kidini.
Iran imetikiswa na wiki kadhaa za maandamano yaliyochochewa na hasira juu ya hali ngumu ya kiuchumi na kisha kugeuka kuwa maandamano makubwa zaidi dhidi ya Jamhuri hiyo ya Kiislamu katika kipindi cha zaidi ya miaka mitatu.
Mamlaka za Iran zimeilaumu Marekani kwa maandamano hayo makubwa ambayo wameyataja kuwa ni ghasia na operesheni za kigaidi.