Israel: Mabaki tuliyokabidhiwa na Hamas sio ya mateka wetu
3 Desemba 2025
Ofisi ya Waziri Mkuu wa Israeli Benjamin Netanyahu imesema imefikia uamuzi huo kufuatia uchunguzi wa vinasaba uliofanwa kwa mabaki hayo. Taarifa hizo zilitolewa kwa Jamaa wa mateka wawili waliouawa ambao miili yao bado ipo katika Ukanda wa Gaza.
Mateka hao walichukuliwa na wanamgambo wa Hamas wakati wa shambulio la Oktoba 7 2023, shambulio lililochochea mgogoro mkubwa, unaoendelea sasa mashariki ya kati. Hata hivyo wanamgambo wa Hamas wamesema tayari mabaki ya mateka mmoja, yamepatikana na tayari serikali ya Israel imefahamishwa na kamati ya kimataifa ya msalaba mwekundu.
Hii si mara ya kwanza mabaki ya mateka yasiyo sahihi kukabidhiwa kwa Israel, matukio kama hayo yaliyoshuhudiwa awali yalisababisha mvutano kati ya Israel na Hamas, huku Israel ikisema Hamas inajikokota katika hatua ya kuirejesha miili hiyo na Hamas nayo ikisema bado, ilikuwa inaitafuta baadhi ya miili iliyoaminika kuwa chini ya vifusi vya majengo yaliyoshambuliwa na Israel, katika Ukanda wa Gaza.
Hadi sasa makubaliano dhaifu ya kusitisha mapigano yanayoungwa mkono na Marekani yamekuwa yakitekelezwa tangu Oktoba 10 kwa lengo la kusitisha vita vilivyodumu kwa zaidi ya miaka miwili.
Qatar kuzishinikiza Israel na Hamas kuanza duru mpya ya mazungumzo
Huku hayo yakiarifiwa Qatar, imesema inatumai pande hizo mbili hasimu, Israel na Hamas wanaweza kurejea katika awamu mpya ya mazungumzo kufikia mpango wa amani ya kudumu katika eneo hilo la wapalestina, kufuatia makubaliano hayo ya Oktoba 10.
Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Qatar Majed al-Ansari, amesema wanafikiria kuwashinikiza kuingia katika awamu ya pili ya majadiliano hivi karibuni.
"Tunafanya kazi kwa karibu sana, na tunafikiri kwamba tunapaswa kuzishinikiza pande zote kufikia hatua ya pili hivi karibuni. Mambo yanayoendelea huenda yakayumbisha makubaliano yaliyopo. Lakini tunaendelea kujitolea na washirika wetu kusonga mbele zaidi na kuhakikisha kwamba tunapata matokeo chanya na kuelekea katika hatua ya pili."
Akizungumza na waandishi habari mjini Doha Al-Ansari, pia alikosoa mashambulizi ya Israel ya mara kwa mara mjini Gaza, licha ya makubaliano hayo yaliyoongozwa na Marekani, Misri na Qatar yenyewe ya usitishwaji mapigano.
Kwengineko Kitengo cha jeshi la Israel kinachosimamia shughuli za kuratibu utoaji msaada Gaza,COGAT, kimesema Israel itafungua kivuko cha Rafah katika siku chache sijazo, kutoa nafasi ya wakaazi wa Ukanda wa Gaza kulitoroka eneo hilo na kuingia nchini Misri.