1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran yatishia kujitoa katika makubaliano ya kinyuklia

Sekione Kitojo
29 Agosti 2018

Kiongozi mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei ameonesha wasiwasi wake juu ya uwezo wa mataifa ya Ulaya kuokoa makubaliano ya  kinyuklia na Iran ya mwaka 2015. Amesema pia Iran huenda ikajitoa pia katika makubaliano hayo.

https://p.dw.com/p/33znz
Iran Teheran - Hassan Rouhani und Ayatollah Ali Khamenei  bei Kabinettssitzung
Picha: ReutersOfficial President.ir Website

Amesema  hayo  kutokana  na  mataifa  yenye  nguvu  ya Ulaya  hivi  sasa  yanakabiliwa na kitisho kufuatia kujitoa  kwa Marekani katika  makubaliano  hayo, na  kusema  Iran huenda  ikajitoa  pia katika  makubaliano  hayo.

Khamenei  amemtahadharisha  rais Hassan Rouhani  kutotegemea mno uungwaji  mkono  wa  mataifa  ya  Ulaya wakati  akijikuta  katika mbinyo  mkali nyumbani  kuhusiana  na  jinsi  anavyoshughulikia changamoto za kiuchumi  baada  ya  Marekani  kurejesha  vikwazo dhidi  ya  nchi  hiyo, na  mawaziri  muhimu  wakishambuliwa  bungeni.

Iran Präsident Hassan Rohani
Rais wa Iran Hassan RouhaniPicha: picture-alliance/AP Photo/V. Salemi

Kufuatia  kujitoa  kwa  rais  wa  marekani  Donald Trump kutoka katika  makubaliano  ya  kimataifa ambayo  yangedhibiti dhamira  ya Iran  kujipatia  silaha  za  kinyuklia, mataifa  yenye  nguvu  ya  Ulaya yamekuwa  yakitapia  kuhakikisha  kwamba  Iran  inaendelea kupata manufaa  ya  kiuchumi yanayohitajika  ili  kuibakisha  katika makubaliano  hayo  ya  kinyuklia.

Lakini  katika  matamshi  yake  yaliyochapishwa  katika  tovuti  yake rasmi  Khamenei  alimwambia  Rouhani  na  baraza  lake  la mawaziri  leo, kwamba hakuna matatizo  kuendelea  na  majadiliano na  kuendelea  na  mahusiano na  Ulaya, lakini anapaswa  kuondoa matumaini  kwao  kuhusiana  na  masuala  ya  kiuchumi  ama makubaliano  ya  kinyuklia.

"Makubaliano  ya  kinyuklia  ni  njia , sio lengo, na iwapo hatutafikia hitimisho  hili , tunaweza  kujitoa," Khamenei alinukuliwa  akisema. Khamenei aliweka  masharti  kadhaa  mwezi  Mei kwa  mataifa yenye  nguvu  ya  Ulaya iwapo  yanataka  kuiweka  Tehran  katika makubaliano  hayo.

USA Donald Trump
Rais wa Marekani Donald TrumpPicha: picture-alliance/newscom/UPI Photo/K. Dietsch

Masharti  ya  Khamenei

Masharti  hayo  ni  pamoja  na hatua  za benki za  Ulaya  kulinda  biashara  na  Tehran  na  uhakikisho wa  mauzo ya  mafuta  ya  Iran.

Akizungumza  katika  mkutano  huo  leo, Khamenei  alisema  Tehran haitafanya  majadiliano  na  maafisa   wa  marekani  wasio na heshima  na  wanaopendelea  mivutano " kufikia  makubaliano mapya  kuhusiana  na  mpango  wake wa  kinyuklia kwasababu Marekani  inataka  kujisifu kwamba  wameweza  kuileta  Iran  katika meza  ya  mazungumzo".

Khamenei amemwambia  Rouhani  na  baraza  lake  la  mawaziri kufanyakazi  , "usiku  na  mchana "  kutatua  matatizo yanayoengezeka  ya  kiuchumi  ambayo  ni  pamoja  na  kuporomoka kwa  sarafu  ya  rial na  kuongezeka  kwa  ukosefu  wa  ajira.

Lakini  wakati  huo  huo  ameonekana  kulitaka  bunge  kutoweka mbinyo  mkubwa  zaidi  dhidi  ya  Rouhani  ambaye  alihojiwa  kwa kiasi  kikubwa  kuhusiana  na  utendaji  wake  kuhusu uchumi. Maafisa  wanapaswa  kujiunga  pamoja  dhidi ya  mbinyo  wa Marekani ambao , alisema , kwa  kuwa  kutangaza  kuwapo  na tofauti kutalifanya  taifa  hilo  kutokuwa  na  furaha  zaidi.

Iran Urananreicherungsanlage Isfahan
Mitambo ya Iran yakurutubisha madini ya urani katika kituo cha IsfahanPicha: Imago

Wakati  huo  huo  mawaziri  kadhaa  wa  serikali  wanatarajiwa kufika mbele  ya  bunge  la  Iran  katika  siku  zinazokuja  wakati wabunge  wanadai  majibu  katika  mzozo wa kiuchumi  wa  nchi hiyo.

Ufaransa  nayo  imewaambia  wanadiplomasia  wake  pamoja  na maafisa  wa  wizara  ya  mambo  ya  kigeni  kuahirisha  moja  kwa moja  safari  ambazo  si  lazima  kwenda  Iran, ikielezea  kuhusu mpango  ulioshindwa  wa shambulio  la  bomu pamoja  na kuongezeka  msimamo  mkali  wa  Tehran  kuielekea  Ufaransa, kwa mujibu wa  waraka  wa  ndani  katika  serikali  ya  Ufaransa.

Mwandishi: Sekione  Kitojo  /  dpae

Mhariri: Iddi Ssessanga