1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUrusi

Zelensky atarajia mazungumzo mapema Machi Abu Dhabi

27 Februari 2026

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky asema duru ijayo ya mazungumzo na Urusi itafanyika mapema Machi Abu Dhabi, huku mashambulizi ya droni na makombora yakiendelea kuathiri maeneo kadhaa nchini Ukraine.

https://p.dw.com/p/59UP9
Lithuania, Vilnius 2026 | Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky katika mkutano na waandishi wa habari pamoja na Gitanas Nausėda na Karol Nawrocki.
Rais Volodymyr Zelenskiy ameeleza matumaini ya kukutana siku moja ana kwa ana na Rais wa Urusi Vladmir Putin.Picha: Kuba Stezycki/REUTERS

Rais Volodymyr Zelensky amesema ana matumaini kuwa duru ijayo ya mazungumzo kati ya Ukraine na Urusi itafanyika mapema Machi mjini Abu Dhabi. Kauli hiyo imefuatia mkutano wa maafisa wa Kyiv na wajumbe wa Marekani mjini Geneva. Zelensky amesema kuna utayari mkubwa zaidi wa mfumo wa mazungumzo ya pande tatu.

Amesema lengo ni kukamilisha masuala ya dhamana za usalama na kuandaa mkutano wa ngazi ya juu. Kyiv imekuwa ikisisitiza kuwa mkutano wa ana kwa ana kati ya Zelensky na Vladimir Putin unaweza kuvunja mkwamo wa muda mrefu. Viongozi hao wawili walikutana mara ya mwisho mwaka 2019.

Malengo mapana ya mazungumzo ya Geneva

Mjadiliana mkuu wa Ukraine, Rustem Umerov, alisema mazungumzo ya Geneva yalizingatia pia ujenzi upya wa Ukraine baada ya vita. Aliongeza kuwa pande hizo zimekubaliana misingi itakayounda makubaliano yajayo. Mazungumzo hayo yalihudhuriwa pia na wajumbe wa Marekani.

Ukraine, Kyiv 2026 | Volodymyr Zelensky na wawakilishi wa Umoja wa Ulaya katika mkutano wa “Coalition of the Willing” | Picha ya skrini ikimuonyesha Friedrich Merz.
Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskiy na viongozi wa Umoja wa Ulaya wakihudhuria mkutano wa “Muungano wa Hiari,” wakati wa mashambulizi ya Urusi dhidi ya Ukraine, mjini Kyiv, Ukraine, Februari 24, 2026.Picha: Ukrainian Presidential Press Service/Handout via REUTERS

Kwa upande wake, Urusi imesema ni mapema kutabiri tarehe ya makubaliano. Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi, Sergei Lavrov, amesema Moscow haina muda maalum bali inalenga kutimiza malengo yake, ikiwemo udhibiti kamili wa eneo la Donetsk mashariki mwa Ukraine.

Wakati juhudi za kidiplomasia zikiendelea, mashambulizi ya kijeshi hayajasimama. Maafisa wa Ukraine walisema Urusi ilirusha mamia ya droni na makombora, na kusababisha majeruhi na uharibifu katika maeneo kadhaa. Licha ya hali hiyo, Zelensky amesema anaamini mkutano wa Abu Dhabi unaweza kuwa hatua muhimu kuelekea kumaliza vita.