1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Viongozi wa EU waendelea na mkutano wao uliojaa "hamaki"

Sekione Kitojo
18 Julai 2020

Viongozi wa Umoja wa Ulaya wanasaka muafaka leo Jumamosi katika siku ya pili ya mkutano wao wa kilele kufikia makubaliano juu ya bajeti ya Umoja huo ya euro trilioni 1.85 pamoja na mfuko wa ufufuaji uchumi ulioathirika.

https://p.dw.com/p/3fXFs
Belgien Brüssel | EU-Gipfel
Picha: Reuters/F. Seco

Majadiliano  hayo yanatuwama zaidi  katika  kutaka  kuzisaidia  zile  nchi zilizoathirika  zaidi  na  kusambaa  kwa  virusi vya corona. Katika  mkutano  huo hali ya wasi wasi iko juu miongoni mwa  viongozi  ambao wamefikia hatua  ya kuchoka  baada  ya miezi  kadhaa  ya  kupambana  na  janga  la  virusi  vya  corona katika  nchi zao.

Belgien Brüssel | EU-Gipfel
Waziri mkuu wa Uholanzi Mark Rutte, (wa pili kulia) akizungumza na waziri mkuu wa Sweden Stefan Lofven, (kulia) kansela wa Austria Sebastian Kurz,(kushoto) na waziri mkuu wa Denmark Mette Frederiksen, (wa pili kushoto)Picha: picture-alliance/AP Photo/F. Seco

Siku  nzima  na  usiku za majadiliano ya  viongozi 27 siku  ya  Ijumaa yaliongeza  tu hali ya kutoridhika kuhusiana  na  vipi  fedha  hizo nyingi  zitatumika na  masharti  gani  yanapaswa  kuwekwa.

Hali "ilikuwa hamaki" wakati  mazungumzo  hayo  yakiendelea , waziri mkuu  wa  Uholanzi Mark Rutte  alisema  baada  ya  mazungumzo  ya muda  mrefu  siku  ya  Ijumaa. "Hii  itachukua  muda  kidogo,  nafikiri."

Halmashauri  ya  utendaji  ya  Umoja  wa  Ulaya  ilipendekeza  mfuko wa  euro  bilioni 750, kwa  sehemu  fulani chini  ya  mfumo  wa kawaida  wa  kukopa,  utakaowekwa  kama  mkopo  na misaada kwa zile  nchi  ambazo zitakuwa  na  uhitaji  mkubwa. Hii  inakuja  juu  ya bajeti  ya  Umoja  wa  Ulaya  ya  miaka  saba  yenye thamani  ya euro  trilioni 1 ambayo  viongozi walikuwa  wakipambana  huku ugonjwa  wa  COVID-19 ukishambulia  bara  lao.

Belgien Brüssel | EU-Gipfel: Angela Merkel, Giuseppe Conte, Mark Rutte und Ursula von der Leyen
Angela Merkel kansela wa Ujerumani (katikati) akizungumza na Giuseppe Conte wa Italia, Mark Rutte wa Uholanzi na Ursula von der Leyen (kulia)Picha: Reuters/F. Seco

Mapendekezo  mapya

Mkutano  huo  uliahirishwa  wakati wa chakula  cha  mchana  leo Jumamosi(18.07.2020) ili kila  ujumbe  uweza  kujadili mapendekezo  mapya  kutoka  kwa  mwenyeji  wa  mkutano  huo Charles Michel, kwa  mujibu wa  mwanadiplomasia  wa  Ulaya.

Mapendekezo  hayo  mapya  yanapunguza  kiwango cha  misaada ya  moja  kwa  moja  katika  mfuko  wa  uokozi na  kupandisha kiwango  cha  mikopo  ambacho  kitahitajika  kulipwa , katika muda ambao  kundi la  mataifa  pinzani  kwa mpango  huo  yakiongozwa na  Uholanzi  yataridhia, amesema  mwanadiplomasia  huyo.

Belgien Brüssel | EU-Ratspräsidenten | Charles Michel
Mwenyeji wa mkutano wa viongozi wa Ulaya rais wa baraza la Ulaya Charles MichelPicha: picture-alliance/AP Photo/F. Seco

Lakini  ufuatiliaji wa fedha  za  uokozi bado  unabaki  kuwa kikwazo kikubwa, mwanadiplomasia  huyo  alisema. Michel alipendekeza hatua  ambayo  haitafika  kuruhusu nchi  yoyote  kutumia  kura ya turufu juu  ya  vipi  serikali  zinaweza  kutumia  fedha  hizo.

Mwanadiplomasia mwingine ameyaeleza mapendekezo  mapya ya Michel  kama  hatua  tu  ya  kwanza  katika  kile  ambacho  kinaweza kuwa  safari  ndefu kuelekea  makubaliano. Wanadiplomasia  wote hao  wamezungumza  kwa  masharti ya  kutotajwa  majina kwasababu  hawakuidhinishwa  kujadili  masuala  hayo yanayojadiliwa  kwa  faragha  kwa  umma.