Vikosi vya Syria vyaendelea kushambulia raia
18 Agosti 2011Assad alitamaka hayo baada ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon, kueleza wasiwasi wake kuhusu ripoti za matumizi ya nguvu na ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu unaofanywa na vikosi vya Syria dhidi ya raia. Lakini wanaharakati wanasema, mashambulio ya vikosi vya serikali yaliendelea wakati wa usiku na waandamanaji 2 waliuawa baada ya kupigwa risasi na wanamgambo wa Rais Assad katika mji wa Homs. Wakati huo huo, vikosi vya usalama vilisaka nyumba katika mitaa ya Hama na mji mkuu Damascus. Licha ya serikali kutangaza kuwa majeshi yameondoshwa kutoka miji ya Hama na Deir al-zor, wakaazi wanasema, vikosi vya kijeshi vimebakia katika miji hiyo na vinaendelea kuwashambulia na kuwakamata wapinzani wa serikali. Majeshi vile vile, yamebakia Homs na katika mji wa bandari Latakia.
Nyumba zasakwa na kamatakamata yaendelea
Kwa mujibu wa wakaazi wa Hama, vikosi vya Syria vilivamia nyumba katika kiitongoji cha al-Qusour wakati wa usiku. Vile vile, polisi na wanamgambo walisaka nyumba katika mtaa wa Rukh al-Din mjini Damascus. Hata kwenye mpaka wa Uturuki, kijiji cha Bdama kilifyatuliwa risasi na vikosi vya serikali, ili kuzuia wakimbizi wa Latakia kwenda eneo hilo la mpakani. Kwa mujibu wa Muungano wa kuratibu mapinduzi ya Syria, hadi raia 24 waliuawa siku ya Jumatano nchini humo. Duru mjini Washington zimenukuliwa zikisema kuwa Marekani inatarajiwa kutoa mwito kwa Rais al-Assad kuondoka madarakani, huku Umoja wa Ulaya ukitazamiwa kufanya hivyo hivyo. Ujerumani imetoa mwito kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kulijadili suala la Syria hii leo.Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Ujerumani, Guido Westerwelle amesema:
"Tunazungumza pia na wanachama wengine katika Baraza La Usalama. Lengo ni kuwa na ujumbe dhahiri wa pamoja kuitaka serikali ya Syria kusitisha matumizi ya nguvu"
Inatathminiwa kuwa hadi raia 2,000 wameuawa katika mashambulio ya vikosi vya serikali, tangu maandamano ya upinzani kuanza miezi mitano iliyopita nchini Syria. Vyombo vya habari vingi vilivyo huru, vimefukuzwa Syria tangu machafuko yalipoibuka, kwa hivyo ni vigumu kuthibitisha ripoti zinazotoka nchini humo. Mkuu wa Shirika la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa, Navi Pillai na Mkuu wa misaada ya kiutu wa Umoja wa Mataifa, Valeria Amos leo watahotubia Baraza la Usalama katika kikao cha faragha. Wanadiplomasia wanasema, Pillai huenda akaliomba Baraza la Usalama kulifikisha suala la Syria katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu.Mwandishi: Martin,Prema/rtre/zpr
Mhariri: Abdul-Rahman