1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ulimwengu waadhimisha miaka mitano ya mkataba wa Paris

12 Desemba 2020

Viongozi wa dunia wanatarajiwa kutangaza malengo mapana zaidi ya kudhibiti ongezeko la joto duniani katika maadhimisho ya miaka mitano ya mkataba wa kihistoria wa kupambana na mabadiliko ya tabianchi wa mjini Paris.

https://p.dw.com/p/3mbnD
Blick vom Fernsehturm Colonius in Köln
Picha: Christoph Hardt/Geisler-Fotopress/dpa/picture alliance

Mkutano wa kilele utakaofanyika leo kwa njia ya mtandao unakuja wakati Umoja wa Mataifa umetahadharisha kuwa ahadi za sasa zilizotolewa na mataifa duniani kuzuia kupanda kwa kiwango cha joto bado hazitoshi.

Uingereza, Ufaransa na Umoja wa Mataifa ndiyo wenyeji wa mkutano huo ambao utafunguliwa rasmi na waziri mkuu wa Uingereza Boris Johnson baadae leo mchana.

Rais wa China Xi Jinpinga na wa Ufaransa Emmanuel Macron ni miongoni mwa viongozi wakuu wa mataifa wanaoshiriki, huku nafasi ya kuzungumza imetolewa kwa viongozi wa mataifa yaliyowasilisha ahadi pana zaidi za kuzuia utoaji wa gesi ya ukaa.

Mataifa hayo yanajumuisha Honduras na Guatemala, ambayo kwa pamoja hivi karibuni yalikumbwa na vimbunga pamoja na India inayokabaliwa na misimu ya mwaka isiyotabirika na uchafuzi mkubwa wa hewa.

Viongozi wa kampuni za biashara waliopangiwa kuzungumza ni pamoja na Tim Cook, afisa mtendaji mkuu wa kampuni ya Apple, ambayo imeahidi uzalishaji na usambazaji wa bidhaa zake utafikia lengo la matumizi ya nishati isiyochafua mazingira ifikapo mwaka 2030.

Ahadi za mkataba wa Paris bado hazitoshi 

Mkataba wa Paris wa mwaka 2015 ulishuhudia mataifa duniani yaliweka ahadi ya kuchukua hatua kubwa kudhibiti kupanda kwa kiwango cha joto chini ya nyuzi 2 Celcius juu kidogo ya ilivyokuwa kabla ya mapinduzi ya viwanda na kujaribu pia kupunguza hadi nyuzi 1.5 Celcius miaka inayokuja.

USA UN Generalsekretär Antonio Guterres
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio GuterresPicha: Getty Images/AFP/J. Samad

Lakini Umoja wa Mataifa umesema chini ya ahadi za sasa sayari ya dunia bado ipo kwenye mwelekeo mbaya wa kupanda kiwango cha joto hadi nyuzi 3C ndani ya karne hii ya 21.

Katika mkutano wa leo mataifa yanatarajiwa kutangaza hatua mpya za kupunguza utoaji wa gesi ya Kaboni, kuweka wazi mikakati ya muda mrefu na ahadi ya msaada wa kifedha kwa mataifa masikini kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Mkutano huo unafanyika siku moja baada ya viongozi wa Umoja wa Ulaya kutangaza jana nia ya kupunguza utoaji wa gesi ya ukaa kwa asilimia 55 ifikapo mwaka 2030.

Uingereza yafunga mkaja kupambana na uchafuzi wa mazingira

Hapo jana pia Uingereza ilitangaza kuwa inasitisha ufadhili kwa sekta ya usafirishaji mafuta ya petroli na kuelekeza uangaji mkono kwa miradi ya nishati salama na yenye  kuzalisha kiwango kidogo cha gesi ukaa.

China Huainan Kohlekraftwerk
Picha: Getty Images/K. Frayer

Waziri mkuu Boris Johnson amesema kupitia uamuzi huo aloutaja kuwa madhubiti Uingereza itatengezena nafasi nyingi za ajira, kufufua uchumi baada ya janga la virusi vya corona na kuilinda sayari ya dunia kwa manufaa ya vizazi vinavyokuja.

Chini ya hatua hiyo serikali mjini London, itasitisha msaada wa kifedha kwa usafirishaji nje bidhaa za mafuta ya petroli pamoja na ruzuku kwa miradi mipya ya mafuta, gesi asili na uzalishaji nishati kwa kutumia makaa ya mawe.

Marekani ambayo ni mtoaji mkubwa namba mbili wa gesi chafuzi nyuma ya China ilijiondoa kutoka mkataba wa Paris chini ya utawala wa rais Donald Trumpanayehoji usahihi wa taarifa za kisayansi kuhusu mabadiliko ya tabianchi.

Hata hivyo rais mteule Joe Biden amekwishaahidi kuwa serikali yake itairejesha chini hiyo kwenye mkataba huo na ameteua John Kerry kuwa mjumbe maalum wa Marekani kuhusu mabadiliko ya tabianchi