Ukraine yashambulia bomba la mafuta karibu na Moscow
1 Novemba 2025
Idara za ujasusi za jeshi la Ukraine, zimesema vikosi vya nchi hiyo vimeshambulia bomba muhimu la mafuta katika jimbo la mji mkuu wa Urusi Moscow ambalo linasambaza mafuta kwa jeshi la Urusi.
Madai hayo yanatolewa mnamo wakati Urusi ikiendeleza kampeni yake ya mashambulizi makubwa ya ndege zisizo na rubani na makombora kwenye miundombinu ya nishati ya Ukraine.
Operesheni hiyo ilitekelezwa jana jioni kulingana na taarifa iliyotolewa kupitia ujumbe uliotumwa kwenye mtandao wa Telegram.
Wakati huo huo wizara ya ulinzi ya Urusi imesema vikosi vyake vimevishinda vikosi maalum vya Ukraine ambavyo vilipelekwa katika uwanja wa vita kwenye mkoa wa mashariki wa Pokrovsk katika jaribio la kuvizuia vikosi vya Moscow kusonga mbele.
Urusi inataka kudhibiti eneo lote la Donbas, ambalo linajumuisha mikoa ya Luhansk na Donetsk. Ukraine bado inadhibiti takriban 10% ya Donbas.