1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yapambana kuwahifadhi wakimbizi

Sabine Kinkartz Iddi Ssessanga
25 Julai 2023

Wakati idadi ya wakimbizi wanaokuja Ujerumani inaongezeka, wengi wa wale waliofika miaka iliyopita bado hawajapata makao yao wenyewe. Bado wanaishi katika makazi ya awali.

https://p.dw.com/p/4ULKo
Deutschland I Gemeinschaftsunterkunft für Geflüchtete in Berlin-Spandau
Katika miji mingi ya Ujerumani, makao ya muda huhifadhi wakimbizi kwa miaka mingi.Picha: Frederic Kern/Geisler-Fotopress/picture alliance

Wito wa msaada unaendelea kuja kutoka manispaa ambazo zinaishiwa nafasi ya kuwapokea watafuta hifadhi na wakimbizi wa vita kutoka Ukraine. Mfano wa hivi karibuni: wilaya ya Fulda katika jimbo la kati la Ujerumani la Hesse.

Miji na manispaa "ziko katika ukomo kamili wa uwezo wao" wa kuhudumia watu "angalau nusu njia kiutu," inasomeka barua kutoka baraza la kaunti kwa serikali za majimbo na shirikisho, ambayo idadi kubwa ya wabunge wa eneo hilo waliidhinisha katikati ya Julai.

"Tunahitaji kuweka ukomo wa idadi ya watu wanaoswasili," alisema msimamizi wa wilaya Bernd Woide, mwanachama wa chama cha mrengi wa kati-kulia, Christian Democratic Union, CDU. "Siyo tu kwamba kuna ukosefu wa chaguzi za malazi - huduma pia zimeenea katika malezi ya watoto, shuleni, matibabu katika maeneo mengine mengi."

Soma pia: Scholz aahidi mshikamano na Italia juu ya sera ya hifadhi

Watafuta hifadhi 300,000 wanatarajiwa mwaka wa 2023

Wakati ni Waukraine wachache tu wanaokuja Ujerumani, idadi ya watu wanaotafuta hifadhi inaongezeka. Ofisi ya Shirikisho ya Uhamiaji na Wakimbizi (BAMF) ilihesabu zaidi ya maombi 162,000 ya hifadhi kuanzia Januari hadi Juni mwaka huu. Watu wengi walikuwa wametoka Syria (takribani 44,000), ikifuatiwa na Afghanistan (takriban 28,000) na Uturuki (karibu 19,000). Takriban watu 20,000 waliokimbia nchi za Afrika wameomba hifadhi nchini Ujerumani.

Symbolfoto BAMF
Ofisi ya Shirikisho ya Uhamiaji na Wakimbizi (BAMF).Picha: Christoph Hardt/Geisler-Fotopress/picture alliance

Hildesheim, Ujerumani inaweza kutarajia takriban watu 300,000 wanaotafuta hifadhi mwaka wa 2023. Watu wanapofika Ujerumani wakitafuta hifadhi, husambazwa kote nchini na lazima wabaki katika eneo hilo maombi yao yanaposhughulikiwa. Tatizo: Vituo vingi vya malazi vimejaa sana wakati mwingi; mara nyingi hakuna nafasi tena.

Kuna 'mgogoro wa kuhama'

Mtafiti wa uhamiaji Boris Kühn, pamoja na Julian Schlicht, ambaye ni mratibu wa msaada kwa wakimbizi wa mji wa kusini mwa Ujerumani wa Tübingen, wamepata maelezo kupitia uchunguzi wa mipangilio ya makazi ya wakimbizi. Kuna "mgogoro wa kuhama." Hivi sasa, asilimia 25 ya watu waliokuja Ujerumani wakati wa wimbi la wakimbizi na wahamiaji mwaka 2015/2016 bado wanaishi katika makazi ya wakimbizi.

Soma pia: Maelfu waomba hifadhi zaidi ya mara mbili Ujerumani

Kuna kitu kama msongamano kwenye mfumo. Hasa katika maeneo ambayo soko la nyumba ni gumu, ni vigumu kwa wakimbizi wanaotambulika kupata vyumba vyao wenyewe. Athari ya mtiririko ni kwamba waomba hifadhi wapya waliowasili hulazimika mara nyingi kukaa katika vituo vya mapokezi kwa wiki kadhaa, badala ya siku chache. Vituo hivi vya mapokezi pia vina mipaka ya uwezo.

Bila shaka kuna tofauti za kikanda. Kühn na Schlicht waliona kuwa miji na manispaa zilizoko chini ya shinikizo zaidi sasa ndiyo iliyofuta nafasi za wafanyakazi katika maeneo ya ujumuishaji au kazi ya kijamii ya wakimbizi, pamoja na miundo kama vile mitandao au mikutano ya mezani katika miaka ya baada ya wimbi la la 2015/2016.

Katika maeneo ambayo mipango na nafasi hizi badala yake viliendelezwa zaidi, mamlaka ziko katika nafasi nzuri ya kushughulikia changamoto mpya iliyoanza mnamo 2022.

Konflikt in Afghanistan - Brandenburg erwartet Ortskräfte
Mojawapo ya vituo vya kuhifadhi wakimbizi katika eneo la Ujerumani Mashariki.Picha: Soeren Stache/dpa-Zentralbild/dpa/picture alliance

Sehemu kubwa ya haya ni suala la utashi wa kisiasa, na vile vile vipaumbele vya kisiasa. "Kuwapa hifadhi wakimbizi ni lazima, lakini kuna nafasi iliyoachwa ya kufanya ujanja katika mfumo wa serikali za mitaa inapokuja jinsi gani hilo linatekelezwa," utafiti ulibainisha.

Changamoto, lakini si kuzidiwa

"Kwa kweli ni suala zito," waandishi waliandika. "Kipindi cha utulivu kinafuatwa - kwa mara ya pili sasa katika muda wa miaka michache - na ujenzi mkali wa makazi ya dharura, maombi ya dharura kutoka kwa utawala na hatimaye mjadala wa mzigo."

Soma pia: Ujerumani kuboresha hatua za usalama

Düsseldorf ni miongoni mwa miji ambayo imefanya vyema zaidi. Ndani ya muda mfupi mwaka wa 2022, wakimbizi 10,000 wa vita kutoka Ukraine waliwasili katika mji mkuu wa jimbo la North Rhine-Westphalia. "Hao walikuwa wakimbizi wengi kuliko miaka ya 2015/2016 pamoja," alisema Miriam Koch, naibu anaehusika na utamaduni na ushirikiano. "Pamoja na hayo, hatukulemewa, bali tulihisi changamoto tu."

Huko Düsseldorf, mamlaka ya jiji hutafuta malazi ya kukodisha kwa wakimbizi wanaotambulika. Hiyo pia ni pamoja na kuwashawishi wamiliki wa nyumba za kibinafsi kukubali wakimbizi kama wapangaji - jambo ambalo mara nyingi ni gumu. Koch anaelezea wamiliki wa nyumba ambao walitaka tu kuchukua wanawake na watoto wa Kiukreni.

Katika hali nyingi, ushawishi mkubwa ulikuwa muhimu ili "kuondoa hofu na wasiwasi" wa wamiliki wa nyumba, kama Koch alivyoweka, na dhana kama vile vipindi vya majaribio vilipaswa kutolewa.

Seehofer aja na mpango wake wa wakimbizi

Katika jimbo la kusini-magharibi la Baden-Württemberg, miji kadhaa imeungana kutafuta makao. Baadhi ya serikali za mitaa hulipia gharama za ukarabati ili kuwezea majengo yalioachwa yatumike, huku nyingine zikiwapa uhakikisho wa kupangisha nyumba au kusaini makubaliano ya ukodishaji kwa miaka michache ya kwanza, kwa lengo kwamba wapangaji wanachukua jukumu hilo baada ya hapo.

Soma pia: Ujerumani, Sweden zina mzigo mkubwa wa wakimbizi

Mariam Koch kutoka Düsseldorf angependa kuona kwamba wakimbizi wote - na siyo Waukraine - wanaweza kuihfadhia katika makazi binafsi. Kuna wahamiaji wengi nchini ujerumani ambao wangekuwa tayari kuwaleta ndugu zao, marafiki au jamaa waliokimbia mataifa yao ya asili.

Wakati huo huo, idadi inayoongezeka ya mamlaka za mitaa wanaomba kupelekewa tu wakimbizi ambao wana matarajio ya kukaa Ujerumani.

Kulingana na takwimu za hifadhi kutoka Ofisi ya Shirikisho ya Uhamiaji na Wakimbizi, takriban maombi 133,000 ya hifadhi yalishughulikiwa na kuamuliwa katika nusu ya kwanza ya 2023. Kati ya haya, asilimia 48 yalikataliwa kwa sababu zinazohusiana na maudhui au kiufundi. Ni kila mwombaji wa pili tu alikuwa na matarajio ya kubaki Ujerumani.