1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Steinmeier: "Demokrasia yetu ni imara"

Bruce Amani
24 Desemba 2018

Rais wa Ujerumani Frank-Walker Steinmeier amewaomba watu wa Ujerumani kuitatua mivutano katika jamii kwa kusemezana. Steinmeier amesema katika hotuba yake ya Krismasi kuwa nchi haipaswi kuachwa itengane

https://p.dw.com/p/3Aa3w
Bundespräsident Frank-Walter Steinmeier Weihnachtsansprache 2018
Picha: Reuters/A. Hilse

Upinzani wa kisiasa na kijamii nchini Ujerumani umeongezeka katika mwaka wa 2018. Kuna mazungumzo mengi ya mgawanyiko wa kijamii, ya utengano kati ya wanasiasa na watu wa kawaida.

Wengi wanaelezea hasira, hasa kwa kile kinachofahamika kama "mitandao ya kimajii”, ambako aghalabu huwa hakuna nia ya kweli ya mjadala au kubadilishana mawazo ya kweli.

Katika hotuba yake ya Krismasi, rais wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier amegusia kuongezeka kwa uchungu katika majadiliano hayo. "Kila mahali unakoangalia –hasa kwenye mitandao ya kijamii – tunaona chuki; kuna kupiga kelele na hasira za kila siku,” alisema. "Nnahisi kuwa sisi Wajerumani tunatumia muda mchache kusemezana sisi wenyewe. Na hata muda mchache Zaidi kumsikiliza kila mmoja.” Steinmeier anawaomba watu kuendelea kusemezana, hata kama wana maoni yanayotofautiana na yanasababisha majibizano – kwa sababu hiyo ndio maana ya demokrasia.

Jihusisheni

"Demokrasia yetu ni imara kabisa!” Amesema rais huyo wa Ujerumani. Anashuhudia hilo kila siku, anaeleza – mamilioni ya watu nchini Ujerumani hufanikiwa katika njia hiyo. Kila mmoja anayesikika katika jamii yake, vyama au mabaraza ya mjini, kila mmoja anayefanya kazi hospitalini na makazi ya kuwalea watu, na polisi au zima moto, pia katika wakati wa Krismasi – wote huchangia kwa hilo.

"Demokrasia yetu kila mara ni imara kulingana na tunavyoitengeneza,” Anasema. "Msingi wake ni kuwa tuyatoe maoni yetu, na kuwa tuko tayari kujadiliana kuhusu tunachokiamini.” Tutetee maoni yetu, wakati tukiheshimu ya wengine: "Kulegeza msimamo na kufikia makubaliano haimaanishi udhaifu, bali ni ishara ya nguvu. Uwezo wa kufikia maelewano ndio uti wa mgongo wa demokrasia.”

Mifano ya tahadhari nje ya nchi

Hii ni hotuba ya pili ya Krismasi ya Steinmeier kwa watu wa Ujerumani, na wakati huu, tofauti na mwaka jana, pia anazitaja nchi nyingine. "Kinachofanyika wakati jamii zinatengana, na wakati upande mmoja unashindwa kuzungumza na mwingine bila hali hiyo kuwa majibizano, kinadhihirika wazi katika dunia inayotuzunguka,”  Anasema. Rais huyo wa Ujerumani anatoa mfano wa "vizuizi vinavyochomwa mjini Paris, mgawanyiko mkubwa wa kisiasa nchini Marekani, na wasiwasi nchini Uingereza kabla ya Brexit,” na kusema kuwa "Ulaya inawekwa katika mtihani nchini Hungary, Italia na maeneo mengine.” Wajerumani, "katikati ya Ulaya, bila shaka hawana kinga dhidi ya matukio haya,” anaonya – akitoa wito wake wa kuwepo mazungumzo, majadiliano na kushikamana.

'Endelea kuzungumza na mwenzako'

"Katika nchi yetu, pia, kuna hali ya sintofahamu, kuna hofu na kuna hasira,” Anasema Steinmeier. Na hii hasa ndio maana amaanimi kuwa mazungumzo wanayokuwa nayo watu katika siku chache zijazo – katika chakula cha jioni cha Siku Kuu ya Krismasi, na jamaa na marafiki – ni muhimu sana. "Naamini ni vizuri kwetu kushiriki katika mdahalo; ni vizuri kwetu kuzungumza na kila mmoja. Kama kuna kitu nnachotamani kwa taifa langu, basi ni: Tuendeleze mjadala!”

'Sisi sote ni sehemu ya nchini hii'

Kinachompa wasiwasi Steinmeier "zaidi ya kupiga kelele kwa baadhi ya watu ni kimya cha wengine wengi." Idadi inayoongezeka ya watu, anasema, wanazingatia tu hali zao na kuishi katika mbingu yao ambayo kila mmoja hukubaliana kwa asilimia 100 – pia na asiyekuwa katika maisha hayo.

Anapinga hali ya aina hiyo ya kujitenga, akisisitiza kuwa "kitu kimoja kinabaki kuwa kweli: sote ni sehemu ya nchi hii, bila kujali asili yetu, rangi ya ngozi, mtazamo wa maisha au timu ya michezo tuipendayo."

Mwandishi: Bruce Amani/dw
https://www.dw.com/en/frank-walter-steinmeier-our-democracy-is-as-strong-as-we-make-it/a-46849802