1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wafaransa waandamana kupinga matukio ya kuwaandama Wayahudi

12 Novemba 2023

Tangu Israel ilipoanzisha mashambulizi dhidi ya Hamas katika Ukanda wa Gaza,visa vya Wayahudi kushambuliwa vimeongezeka Ufaransa

https://p.dw.com/p/4YiuW
Viongozi mbali mbali wakishiriki maandamano ya kupinga chuki dhidi ya wayahudi,mjini Paris,12.11.2023
Maandamano ya kupinga chuki dhidi ya Wayahudi UfaransaPicha: Claudia Greco/REUTERS

Rais Emmanuel Macron amewatolea mwito wananchi wa Ufaransa kusimama kidete dhidi ya vitendo vya chuki dhidi ya wayahudi. Macron ametoa mwito huo kabla ya maandamano makubwa yaliyofanyika katika mji mkuu Paris leo Jumapili ya kupinga ongezeko la matukio ya chuki dhidi ya Wayahudi.

Waziri mkuu Elisabeth Borne na wanasiasa wengine mbali mbali walitarajiwa kushiriki maandamano hayo huku serikali ikiwa imetuma askari 3,000 kulinda usalama.

Maandamano hayo yameitishwa na viongozi wa baraza la Seneti na bunge la Ufaransa kufuatia kuongezeka kwa kasi vitendo vya kuwaandamana Wayahudi nchini humo,tangu Israel ilipoanzisha vita vyake dhidi ya kundi la Hamas katika Ukanda wa Gaza.

Mamlaka za Ufaransa zimeshapokea  zaidi ya matukio 1,000 ya kuandamwa Wayahudi kote nchini humo katika kipindi cha mwezi mmoja.Rais Emmanuel Macron amewatolea mwito wananchi kubakia na mshikamano wa kuheshimu maadili ya taifa na kwamba Ufaransa haiwezi kuvumilia raia wenzao, Wayahudi  kuishi kwa uwoga  ndani ya nchi yao.

Kiongozi wa chama cha mrengo wa siasa kali,cha National Rally, Marine Le Pen, alitazamiwa pia kushiriki maandamano hayo kutokana na kukosolewa chama hicho kwamba, kimeshindwa kujitenga na mitizamo yake ya chuki dhidi ya wayahudi, licha ya kuzidi kuungwa mkono kisiasa.