Majaribio ya kwanza ya chanjo ya Covid-19 njiani
25 Machi 2020Kampuni hiyo inamilikiwa kwa sehemu kubwa na tajiri Dietmar Hopp na hivi karibuni imetoa matumaini kuwa chanjo ya virusi vya Corona inaweza kupatikana kufikia majira ya mapukutiko mwaka 2020 ikiwa kila mpango utakwenda kama ulivyo. Kwa hiyo kimsingi matarajio ya chanjo mpya ni kati ya mwezi Septemba hadi Disemba mwaka huu,
Lakini hadi sasa ni hatua kiasi gani imepigwa kuelekea kupatikana chanjo hiyo.
Mkemia Friedrich von Bohlen ambaye ni mjumbe wa bodi ya kampuni ya CureVac amesema kampuni hiyo mbali ya kuwekeza nguvu kutafuta chanjo, wanafanya pia tafiti ya tiba dhidi ya ugonjwa wa COVID-19.
Kimsingi chanjo ni njia pekee ya kuwalinda watu dhidi ya maambukizi lakini kwa wale waliokwisha ambukizwa tayari wanahitaji tiba ambayo kwa bahati mbaya hadi sasa haipo.
Licha ya kuwa wanasayansi wanafahamu kuwa ugonjwa wa COVID-19 unaweza kusababisha homa kali ya mapafu, wataalamu bado hawajafanikiwa kwa uhakika kupata dawa itakayopunguza uvimbe kwenye mapafu.
Kwa hiyo ni muhimu kutanabaisha kuwa wakati wanasayansi wanatafuta chanjo dhidi ya virusi vya corona wanawajibika pia kutafuta tiba ya kuwaokoa maelfu ya watu wanaokumbwa na ugonjwa wa COVID-19.
Kulingana na Bohlen utafutaji wa chanjo bado ni kipaumbele na kuna mafanikio kadhaa yamekwishapatikana na hivi karibuni wataanza kufanya majaribio ya sampuli kadhaa za chanjo kwenye maabara.
Kwa msaada wa teknolojia ya kisasa, wataalumu wanalenga kutumia sehemu ya kiinitete cha seli ya binadamu kama chanzo cha taarifa muhimu katika kutengeneza chanjo dhidi ya virusi vya Corona ambavyo hushambulia seli za mwili wa aliyeambukizwa.
Watu wengi hasa barani Ulaya taarifa za maendeleo hayo ni muhimu, kanuni za kuwalazimisha watu kujitenga na kuzuia mikusanyiko kutokana na wasiwasi wa kusambaa virusi vya Corona zimeanza kuwachosha wakaazi wa bara hilo hususan katika wakati ambapo msimu wa majira ya kiangazi unakaribia.
Lakini wataalumu wametahadharisha bado ni mapema mno kushusha pumzi. Suala la kutafuta chanjo au tiba linajumuisha masuala chungu nzima ambayo wakati mwingine ni ngumu kutabiri jinsi yatakavyokwenda.
Baada ya kutengeneza na kufanyiwa majaribio ya maabara chanjo na tiba zinapaswa kufanyiwa majaribio kwenye miili ya watu na kuthibitisha uwezo wake wa kufanya kazi na tathmini nyingine nyingi ambazo wadhbiti wa ubora wanapaswa kuzingatia.
Kadhalika pindi zikipatikana zitahitaji ithabiti ya kuanza uzalishaji wake kwa wingi na kusambazwa ili zianze kutumika kwa wenye uhitaji. Ndiyo maana pamoja na matumini ya kuanza majaribio wataalumu wengi wanaweka muda wa hadi mwaka mmoja kabla chanjo kamili dhidi ya Corona kuanza kutumika kote ulimwenguni.
Janga la Corona na juhudi za kutafuta kinga na matibabu yake limezusha mjadala mpya barani Ulaya na bila shaka kote ulimwengu. Biyoteknolojia na kampuni zinazotumia muda mwingi kusaka suluhu ya janga hilo siyo mashuhuri sana mbele ya umma au machoni mwa wanasiasa na watunga sera.
Ingawa wanasayansi wa nchini Ujerumani kama mkemia Bohlen wanaridhishwa na mchango wa serikali katika kufadhili tafiti za msingi za tiba ya umma, wengi bado wana fikra kuwa serikali barani Ulaya zinapaswa kutoa msukumo zaidi kwenye kuzipiga jeki kampuni binafsi zinazofanya utafiti.
Tafiti na gunduzi yingi zinashindwa kufikia matokeo ya maana kwa sababu watu binafsi hawana mitaji ya kutosha kuendeleza kile walichogundua.
Mifumo ya tiba mamboleo inayotegemea sana teknolojia ni tofauti na tiba zilizozoeleka. Hivi sasa ugunduzi wa magonjwa na matibabu unaweza kufanyika kwa kutumia mbinu tofauti za kimaabara zilizochochewa na ubunifu na wanasayansi wa Ujerumani wanadhani taifa hilo halifanyi vya kutosha kusaidia mchakato huo.
Mlipuko wa virusi vya Corona umefichua hilo kwa uwazi kabisa.
Bohlen amesema Ujerumani inapaswa kuhakikisha kampuni zinazobuni na kutumia teknolojia ya kisasa kutafuta majibu ya matatizo ya kiafya zinaundwa au kuwa na makao yake nchini humo.