1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kanisa Katoliki Tanzania: Kuua waandamanaji ni aibu kwa nchi

11 Novemba 2025

Askofu, Ruwa'ichi amesema nchi imejeruhiwa na watu waliuawa kiholela kwa sababu ya kuandamana ilhali adhabu ya kuandamana sio kifo cha risasi.

https://p.dw.com/p/53OJq
Tanzania Dar es Salam 2025 | Askofu mkuuJude Thadeus Ruwa'ichi akiongoza ibada
Kanisa Katoliki Tanzania lalaani mauaji ya waandamanaji TanzaniaPicha: Ericky Boniphace/DW

Mamia ya watu walikusanyika leo kanisani kwa ibada ya kuwaombea waliouawa na vikosi vya usalama wakati ya machafuko ya uchaguzi wa Oktoba 29 nchini Tanzania, huku askofu mkuu wa kanisa Katoliki nchini humo Jude Thaddaeus Ruwa'ichi aliyeongoza ibada hiyo, akisema taifa lilipoteza heshima.

Askofu, Ruwa'ichi amesema nchi imejeruhiwa na watu waliuawa kiholela kwa sababu ya kuandamana ilhali adhabu ya kuandamana sio kifo cha risasi.

"Kuna watu waliouawa wakiandamana. lakini adhabu ya kuandamana si kifo cha risasi. Wako watu waliouawa wakiwa majumbani. wamefuatwa wakauawa wakiwa majumbano kwao. Hilo halionyeshi sura ya Tanzania hata kidogo," amesema Ruwa'ichi.

Rais Samia Suluhu Hassan alitangazwa mshindi wa uchaguzi huo kwa kupata asilimia 98 ya kura.

Lakini uchaguzi huo ulipingwa na kusababisha maandamano  katika maeneo mengi ya nchi hiyo ya Afrika Mashariki, huku vikosi vya usalama vikitumia nguvu kuzima maandamano.

Vikosi hivyo vimelaumiwa kuua mamia ya waandamanaji.

Serikali haijatoa takwimu rasmi ya vifo, huku Rais Samia akilaani tu machafuko na kulipongeza jeshi la polisi.