1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Biden kuwataka Wamarekani kuvaa Barakoa kwa siku 100

4 Desemba 2020

Rais Mteule Joe Biden amesema atawaomba Wamarekani kuvaa barakoa kwa hiyari kwa siku 100, lengo likiwa ni kupunguza kasi ya maambukizi ya virusi vya corona.

https://p.dw.com/p/3mDcA
USA Joe Biden mit Atemschutzmaske in Wilmington, Delaware
Picha: Jonathan Ernst/REUTERS

Rais Mteule Joe Biden amesema atawaomba Wamarekani kuvaa barakoa kwa hiyari kwa siku 100, lengo likiwa ni kupunguza kasi ya maambukizi ya virusi vya corona, katika jitihada hizo pia anataka mshauri wa serikali wa masuala ya tiba Dokta Anthony Fauci kusalia katika wadhfa huo.

Kimsingi, Joe Biden amepanga kutoa agizo, litakalowalazimisha Wamarekani kuvaa barakoa katika majengo ya umma, vyombo vya usafiri wa umma, vikiwemo mabasi, ndege na treni katika siku 100 za urais wake. Baada ya sikukuu ya mapumziko, ijulikanayo kama "Mapumziko ya Shukrani" ya juma lililopita, kumekuwa na ongezeko la maaambukizi na vifo vipya katika karibu maeneo yote ya Marekani.

Hadi wakati huu kunatajwa kuwa na wagonjwa zaidi ya 100,000 katika hospitali mbalimbali, kutokana na maambukizi ya virusi, kiwango hicho kikitajwa kuwa kikubwa kuliko katika kipindi chochote kwa wakati huu wa janga la corona. Kwa kila siku taifa limekuwa likiripoti visa vipya vya zaidi ya watu 210,00, ikiwa sambamba na idadi ya vifo 2,907 iliyorekodiwa Alhamis.

Biden ataka mkuu wa Taasisi ya Taifa ya Kukabiliana na Magonjwa ya Kuambukiza Dk. Anthony Fauci kuendelea

USA Dr. Anthony Fauci
Mkuu wa Taasisi ya Taifa ya Udhibiti wa Magonjwa ya Kuambukiza Anthony FauciPicha: picture-alliance/AP Photo/K. Dietsch

Katika mahojiano, yake ambayo alitanabaisha mipango ya kukabiliana na janga hilo, Joe Biden pia alisema anataka kumtumia mtaalamu wa magonjwa ya kuambukiza Dokta Anthony Fauci kuendelea kuwa mkuu wa Taasisi ya Taifa ya Magonjwa ya Kuambukiza. Biden alisema amemuomba asalie katika nafasi yake, ambayo amekuwa akihudumu kwa marais kadhaa waliopita na vile vile kuwa mshauri wake wa masuala ya tiba. Na pia kuwa sehemu ya timu maalumu ya kukabiliana na COVID.

Rais wa sasa na wa zamani kushiriki kupata chanjo kwa hamasa

Katika kufanikisha jitihada ya vita dhidi ya virusi vya corona kwa vitendo rais huyo mteule wa Marekani amesema yupo tayari kushiriki kupatiwa chanjo ya virusi hivyo hadharani kwa lengo la kutoa hamasa ya matumizi yake kwa umma wa Wamarekani. Marais wa zamani Barack Obama, George W. Bush na Bill Clinton nao wamesema wapo tayari kupata chanjo hiyo.

Akizungumza katika kituo kimoja cha radio nchini humo Rais Obama alisikika akisema kama Fauci atamwambia kama chanjo hiyo ni salama, na inakinga atashiriki. Na pia kuahidi kwamba atakifanya kitendo hicho hadharani kwa lengo lile lile la Biden la kuhamasisha umma na kuonesha kwamba yeye ni miongoni mwa wanaoiamini chanjo hiyo.

Soma zaidi:Barr: Hakuna ushahidi wa madai ya wizi wa kura Marekani

Chanjo ambayo imevumbuliwa kwa ushirikiano wa makampuni BioNtech-Pfizer na Moderna-NIH inatarajiwa kuidhinishwa baadaye mwezi huu. Hapo jana mwanasayansi wa juu kabisa alisema inatarajiwa kuwakinga watu milioni 100 ikiwa karibu theluthi moja ya idadi jumla ya watu ifikapo Februari

Vyanzo: kbd/nm (AFP, AP, Reuters)