1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Guterres asema hali ya Gaza "inatisha na haikubaliki"

17 Septemba 2025

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres amekosoa kwa matamshi makali kile amekitaja kuwa "mwenendo wa Israel wa kuutanua mzozo wa Ukanda wa Gaza".

https://p.dw.com/p/50aQI
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres.Picha: Jason DeCrow/AP/picture alliance

Hilo ni baada ya hapo jana Jumanne Israel kuanza operesheni ya ardhini ndani ya mji mkubwa wa ardhi hiyo ya Wapalestina.

Guterres amesema kile kinachoendelea Gaza "kinatisha" akitolea mfano wa uharibifu mkubwa wa makaazi ya Wapalestina na kuongeza kwamba "matendo ya Israel kwenye eneo hilo hayana uhalali na hayavumiliki."

Matamshi hayo ameyatoa  wakati jopo huru la uchunguzi la Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa limetoa ripoti jana Jumanne iliyohitimisha kuwa Israel inafanya mauaji ya halaiki dhidi ya  Wapalestina.

Ripoti hiyo yenye kurasa 72 imeorodhesha ushahidi unaoihusisha moja kwa moja serikali ya Israel na jeshi la nchi hiyo kuwa dhamira ya "kuwaangamiza Wapalestina".

Israel imepuuzilia mbali ripoti hiyo na kuitaja kuwa sehemu ya kampeni chafu ya kulipaka tope taifa hilo la kiyahudi.