1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

EU yataka China iwekewe vikwazo kuhusu suala la Uighur

Bruce Amani
20 Desemba 2019

Bunge la Ulaya limetoa wito wa kuwawekea vikwazo maafisa wa China kuhusiana na suala la watu wa jamii ya wachache ya Waighur. Hii ni hatua mpya dhidi ya serikali ya China

https://p.dw.com/p/3V86V
China Uiguren in der Provinz Xinjiang
Picha: AFP/G. Baker

Katika azimio lililopitishwa jana, wabunge wa Ulaya wamesema mbinu zilizotumiwa mpaka sasa na Umoja wa Ulaya hazijaleta mafanikio yoyote kuhisiana na rekodi ya haki za binaadamu ya China ambayo wanasema imekuwa mbaya Zaidi katika mwaka uliopita.

Taarifa iliyotolewa na Bunge la Ulaya lenye makao yake mjini Strassbourg imesema wabunge wamelitaka Baraza la Ulaya kutangaza vikwazo na kukamata mali za maafisa wa China ambao wanahusika na utesaji mbaya Zaidi wa haki za msingi katika jimbo la Xinjiang.

Wabunge hao wameitaka serikali ya China kusitisha vitendo vya kuwakamata watu kiholea bila kuwafungulia mashitaka au kuhukumiwa kwa makossa ya uhalifu na kuwaachia huru mara moja na bila masharti watu wote walioko kizuizini, akiwemo mshindi wa mwaka huu wa Tuzo ya Sakharov, Ilham Tohti.

Sacharow-Preis für geistige Freiheit 2019 Ilham Tohti
Binti ya mwanaharakati Ilham Tohti akipokea tuzo ya SakharovPicha: Reuters/V. Kessler

Viongozi wa UIaya wanaweza kuamua kutangaza vikwazo hivyo, lakini bunge la Umoja wa Ulaya halina mamlaka ya kufanya hivyo. China ndio mshirika wa pili mkuu wa Umoja wa Ulaya kibiashara, lakini mahusiano yametiwa katika mtihani kutokana na sera ya China katika jimbo la Xinjiang na kutokana na machafuko mjini Hong Kong, miongoni mwa masuala mengine.

China inakabiliwa na shutuma kali kutoka jamii ya kimataifa kwa kuwakusanya karibu watu milioni moja wa kabila la Wauighur na makabila mengine ya wachache wengi wao wakiwa Waislamu na kuwazuilia makambini.

Seirkali ya China awali ilikana kuwepo kambi hizo, lakini sasa inasema ni vituo vya mafunzo ya kiufundi, ambayo ni muhimu katika kupambana na ugaidi.

Mwezi uliopita, gazeti la Marekani la New York Times lilipata nyaraka 403 zinazoonyesha ukandamizaji unaofanywa dhidi ya jamii za walio wachache wengi wao Waislamu katika jimbo hilo, zikiwemo hotuba ambazo hazikuchapishwa za Rais wa China Xi Jinping ambaye aliwataka maafisa kutoonyesha kabisa huruma dhidi ya watu wenye itikadi kali.

Mnamo siku ya Jumatano wiki hii, Bunge la Ulaya lilimkabidhi tuyo ya haki za binaadam binti ya msomi kutoka jamii ya Waighur aliyefungwa jela Ilham Tohti. Jewher Ilham aliipokea Tuzo hiyo ya Sakharov kwa niaba ya baba yake, ambaye ni profesa wa masuala ya kiuchumi anayesifiwa sana na bunge la Ulaya kuwa "sauti ya maridhiano” lakini anashutumiwa na seirkali ya China kuwa "gaidi.”