1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Biden alaani 'sumu' ya itikadi ya watu weupe

Bruce Amani
18 Mei 2022

Rais Joe Biden wa Marekani amekemea kile alichokiita kuwa ni sumu ya itikadi kali ya watu weupe iliyosababisha mauaji ya watu wengi waliofyatuliwa risasi mjini Buffalo, New York.

https://p.dw.com/p/4BRhu
Buffalo I Biden kritisiert  Ideologie von Rechten
Picha: Andrew Harnik/AP/dpa/picture alliance

Akizungumza mjini Buffalo, mji ambao kijana wa kizungu anatuhumiwa kwa kuwauwa Wamarekani weusi 10 katika duka moja kubwa, Biden alisema kilichotokea ni ugaidi wa ndani. "Tuna sheria za kutosha za kushughulikia kinachoendelea sasa. Sehemu ya kile ambacho nchi inapasw akufanya ni kutizama kwenye kioo na kuukabili ukweli. Tuna tatizo la ugaidi wa ndani. Ni la kweli. Najua watu hawataki kunisikia nikisema hilo. Wanasema, yeye ni rais, ni Mdemokrat. Lakini hicho ndicho kamati ya ujasusi imekuwa ikisema. Ndicho jeshi lilikuwa likisema kwa muda mrefu."

USA | Schießerei in einem Supermarket in Buffalo
Mshambuliaji aliwalenga Wamarekani weusiPicha: Matt Rourke/AP Photo/picture alliance

Katika hotuba yake kali ambayo pia ilitoa wito wa kuwekwa vizuizi vya umiliki wa bunduki za rashasha, Biden aliwaorodhesha wahanga, akijizuia kutokwa na machozi wakati akikumbusha jinsi mmoja wa waliouawa, kwa jina Andre Mackniel, mwenye umri wa miaka 53 ambaye alikuwa akinunua keki kwa ajili ya mwanawe wa kiume mwenye umri wa miaka mitatu, wakati mshambuiliaji huyo alipoingia dukani hapo.

Matamshi makali ya Biden yalielekezwa kwa kile alichokielezea kuwa ni "itikadi potovu" ya watu weupe ambayo polisi wanasema ilichochea mshukiwa huyo.

Biden alielezea chuki ambayo kupitia vyombo vya habari na siasa na mtandao wa intaneti imeingia katika vichwa vya watu wenye hasira, waliotengwa na waliopotea na kuwafanya waamini kwa uwongo kuwa uwepo wao utaondolewa na kujazwa na watu wengine.

Mapema jana, Biden, na mkewe Jill Biden, waliweka shada la mauwa nje ya duka kubwa ambako mauaji hayo yalitokea. Kisha akafanya mikutano ya faragha ba jamaa za wahanga na maafisa wa uokozi. Polisi imesema mshukiwa Pyton Gendron, mwenye umri wa miaka 18, alipanga shambulio hilo la ufyatuaji risasi kwa miezi kadhaa na kulichunguza eneo hilo kabla, kulingana na mfululizo wa ujumbe uliohusishwa naye kwenye mitandao ya kijamii.

Buffalo I Biden kritisiert  Ideologie von Rechten
Biden alikutana na jamaa za wahanga wa shambulioPicha: Scott Olson/AFP/Getty Images

Gendron kwanza aliandika kuhusu kuwauwa watu Weusi mwezi Desemba na kuamua kulilenga duka hilo la Buffalo kutokana na idadi kubwa ya Wamarekani Weusi walioko eneo hilo. Hayo ni kwa mujibu wa vyombo yva habari vya Marekani na mamia ya kurasa za ujumbe.

Alikumbusha kuwa alirejea kutoka Maisha ya kustaafu ili kukabiliana na Donald Trump katika uchaguzi wa 2020 baada ya kushangazwa kuwa Trump alikataa kulaani waziwazi Wanazi mamboleo waliokuwa wanaandamana mjini Charlottesville, jimboni Virginia.

Rais Biden amesema demokrasia iko hatarini kuliko wakati mwingine wowote maishani mwake. Chuki na hofu vimepewa oksijeni nyingi na wale wanaojifanya wanaipenda Marekani. Hawaielewi Marekani. Amesema.

AFP