1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Baadhi ya mataifa ya Kiarabu yanaiunga mkono Israe si Iran?

John Juma
16 Aprili 2024

Baadhi ya wachambuzi wanauona ukweli kwamba baadhi ya mataifa ya kiarabu yaliisaidia Israel na Marekani katika kuzima mashambuzlizi ya Iran ya mwishoni mwa juma lililopita. Lakini nchi kama Jordan hali ni tofauti.

https://p.dw.com/p/4eqqa
Iran, Israel | Sanaa ya ukuani ikionesha mzozo wa Mashariki ya Kati
Sanaa ya ukuani ikionesha mzozo wa Mashariki ya KatiPicha: Morteza Nikoubazl/NurPhoto/picture alliance

Iran ilirusha zaidi ya droni na makombora 300 usiku wa kuamkia Jumapili kuelekea Israel, kulipiza kisasi baada ya Israel kushambulia ubalozi mdogo wa Iran ulioko mji wa Damascus mwanzoni mwa mwezi Aprili.

Wakati droni na makombora hayo yalikuwa angani, washirika wa Israel waliingilia kati na kuisaidia Israel. Je ni kwa nini mataifa ya kiarabu yalionekana kuisaidia Israel?

Vikosi vya Marekani na Uingereza vilihusika katika kudungua makombora ya Iran yaliyoelekezwa Israel. Ufaransa pia ilihusika kwa kushika doria katika kanda hiyo ingawa haikubainika wazi ikiwa vikosi vyake vilidungua zana za angani za Iran.

Lakini kile kilichowavutia wengi ni kwamba jeshi la anga la Jordan lilifungua anga yake kwa ndege za Israel na Marekani, na ilionekana kutungua droni za Iran zilizokuwa zikivuka anga yake kuelekea Israel.

Soma pia:Israel yaapa kulipiza kisasi dhidi ya Iran

Kulingana na shirika la habari la Reuters, wakaazi walisikia milio ya miripuko ya silaha nzito angani na picha za mabaki ya droni zilizodunguliwa katika mji mkuu Amman, kusini mwa Jordan zikisambazwa katika mitandao ya kijamii.

Huenda nchi za kiarabu katika eneo la Ghuba, ikiwemo Saudi Arabia zilihusika pia kwa njia isiyo ya moja kwa moja, ikizingatiwa zinahifadhi mifumo ya ulinzi ya mataifa ya Magharibi, ikiwemo pia mifumo ya uchunguzi na vituo vya mafuta ya ndege.

Kulingana na jarida la Uingereza "The Economist” vituo hivyo vyote vingekuwa muhimu katika juhudi za kuzima mashambulizi hayo.

Wachambuzi: Israel haipo peke yake Mashariki ya Kati

Mitandaoni, baadhi ya wachambuzi kama vile mwandishi wa gazeti la  Haaretz,  Anshel Pfeffer na Mairaz Zonszein wa shirrika la kimataifa la kudhibiti  Migogoro, walishangilia ushiriki wa mataifa ya Kiarabu.

Walisema hatua hiyo ilithibitisha kuwa Waarabu na Waisraeli watafanyakazi pamoja na kwamba Israel haipo peke yake Mashariki ya Kati.

Berlin, Ujerumani | Maandamano ya kuonesha mshikamano kwa Israel
Waandamanaji mjini Berlin yakionesha mshikamano kwa IsraelPicha: Jörg Carstensen/dpa/picture alliance

Mkurugenzi wa mpango wa Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini katika Baraza la Ulaya la Mahusiano ya Kigeni, Julien Barnes-Dacey, alithibitisha katika taarifa kwamba mashambulizi ya Iran pia yalipata uungwaji mkono wa kimataifa kwa Israel, ikiwa ni pamoja na mataifa muhimu ya Kiarabu yanayokosoa mashambulizi ya Gaza.

Kwa mfano Jordan, imekuwa mkosoaji mkubwa wa kampeni ya kijeshi ya Israel katika Ukanda wa Gaza.

Soma pia:Viongozi wa dunia waihimiza Israel kutolipiza kisasi

Moja kati ya watu watano nchini Jordan ana asili ya Palestina, akiwemo Malkia mwenyewe wa taifa hilo. Katika muda wa wiki chache zilizopita, kumekuwa na maandamano makubwa Jordan dhidi ya Israel.

Kwa mamlaka za Jordan zinazotizama Marekani kuwa mshirika wa karibu, ni lazima iweke kwenye mizani masilahi yaliyomo, utulivu wake kisiasa na ulinzi wake wenyewe. Jordan ilisema kwa haraka kwamba kwa kuisaidia Israel, ilikuwa inajilinda yenyewe.

Kwenye taarifa, serikali ya Jordan ilisema baadhi ya vifaa vilivyokiuka anga yake vilidunguliwa kwa sababu vilikuwa tishio kwa watu na maeneo yenye wakaazi wengi.

Nafasi ya Saudi Arabia katika mzozo

Saudi Arabia ni nchi nyingine inayolazimika kusawazisha masilahi yake yenyewe, ushirikiano wa kimataifa na siasa kuhusu Gaza.

Taifa hilo tajiri la Ghuba lilitarajiwa kurejesha uhusiano wake wa kawaida na Israel kabla ya shambulizi la Oktoba 7 lililofanywa na wanamgambo wa Hamas kusini mwa Israel na kusababisha takriban vifo vya watu 1,200.

Lakini baada ya Israel kuanzisha mashambulizi ambayo hadi sasa yameua zaidi ya watu 33,000 kulingana na wizara ya Afya inayodhibitiwa na Hamas, mipango ya Saudia ilisitishwa.

Iwe waliingilia kati mashambulizi ya Iran kwa niaba ya Israel mwishoni mwa juma au la, Wasaudia wana sababu nyingine za kuwa tayari kuyadunguwa  makombora ya Iran.

Soma pia:Guterres: Mashariki ya Kati iko katika ukingo wa vita

Kwa miongo kadhaa, kanda ya Mashariki ya Kati imegawanyika kwa misingi ya madhehebu ya kidini. Mataifa yaGhuba ya Kiarabu na idadi kubwa ya Waislamu wa madhehebu ya sunni wakikabiliana dhidi ya Iran, ambayo ina Waislamu wengi wanaofuata  mashehebu ya Shia.

Kimsingi, uadui unaweza kuonekana kuwa sawa na migogoro ya awali katika Ulaya, wakati madhehebu mawili tofauti ya Ukristo - Waprotestanti na Wakatoliki, walipokuwa wakitofautiana.

Nchi za Mashariki ya Kati kama vile Iraq, Syria na Lebanon, ambazo wakaazi wao ni mchanganyiko wa Waislamu wanaofuata madhehebu ya Sunni, pamoja na dini nyingine na makabila mengine, zimejikuta  katikati huku Iran na mataifa ya Ghuba yakijaribu kujenga ushawishi huko.